Dodoma, Namungo vita ya pointi tatu za heshima
Muktasari:
- Dodoma Jiji inaingia kwenye mchezo huo ikiwa nafasi ya tisa kwenye msimamo wa ligi ikikusanya pointi saba baada ya kucheza mechi tano, ikishinda mbili, sare moja na kupoteza mbili, huku ikifunga mabao matatu na kufungwa manne.
VITA ya pointi tatu na heshima inatarajiwa kurindima usiku wa leo Ijumaa, Septemba 11, 2026, wakati Dodoma Jiji FC itakapoikaribisha Namungo FC kwenye Uwanja wa Jamhuri, Dodoma, kuanzia saa 1:00 usiku ikiwa ni mwendelezo wa Ligi Kuu Bara.
Dodoma Jiji inaingia kwenye mchezo huo ikiwa nafasi ya tisa kwenye msimamo wa ligi ikikusanya pointi saba baada ya kucheza mechi tano, ikishinda mbili, sare moja na kupoteza mbili, huku ikifunga mabao matatu na kufungwa manne.
Namungo yenyewe ipo nafasi ya 11 ikiwa na pointi sita baada ya kucheza mechi sita, ikishinda mbili na kupoteza nne, huku ikifunga mabao sita na kufungwa 10.
Licha ya tofauti ndogo ya pointi, mchezo huo unaonekana kuwa na uzito mkubwa kwa timu zote mbili, hasa kutokana na mwenendo wao wa hivi karibuni.
Chini ya Kocha Mkuu, Vincent Mashami, Dodoma Jiji imeanza kupata kasi baada ya kukusanya pointi sita ikishinda mechi mbili mfululizo zilizopi, kufuatia kuanza na sare, kisha vipigo viwili mfululizo.
Ushindi wa mwisho Dodoma Jiji iliupata nyumbani ambako iliichapa Mashujaa FC bao 1-0, matokeo yanayowapa wenyeji matumaini ya kuendeleza ubabe mbele ya mashabiki wao.
Sasa Mashami anataka ushindi mwingine ili kuifanya Dodoma Jiji kufikisha pointi 10 na kusogea zaidi juu kwenye msimamo.
“Tunahitaji kuendelea kufanya vizuri hasa katika mechi za nyumbani, hatutaki kuruhusu kuangusha pointi tunapokuwa uwanja wa nyumbani,” amesema Mashami.
Lakini kazi hiyo haitakuwa rahisi kutokana na Namungo kuingia uwanjani ikiwa na kiu ya kuvunja mfululizo mbaya unaoendelea.
Namungo, chini ya Kocha Mkuu Juma Mgunda, ilianza msimu kwa kasi kwa kushinda mechi zake mbili za kwanza, lakini mambo yamebadilika baada ya timu hiyo kupoteza mechi tatu mfululizo.
Katika mechi hizo, Namungo ilifungwa 2-1 na JKT Tanzania, ikapoteza 3-2 dhidi ya Singida Black Stars, kisha ikalala 2-0 na Azam FC.
Hivyo, mchezo wa leo ni nafasi ya Mgunda kurejesha utulivu kwenye kikosi chake na kuzuia presha kuongezeka zaidi kwenye benchi la ufundi.
Namungo ikishinda itafikisha pointi tisa na kuvunja mfululizo wa vipigo vitatu, huku ikipata nafasi ya kujiweka katika mazingira mazuri zaidi kwenye msimamo.
Hata hivyo, kipigo kingine kitakuwa pigo kubwa kwa timu hiyo kwani kitakuwa cha nne mfululizo na huenda kikaongeza presha kwa Mgunda na wachezaji.
Mgunda amesema “matokeo si mazuri, tunaendelea kuimarisha kikosi na naamini tutafanya vizuri kuanzia mchezo huu.”
Historia ya kukutana kwa timu hizi mbili inaonyesha ushindani mkali, huku zikiwa zimekutana mara 12 katika Ligi Kuu. Namungo imeshinda michezo mitano, Dodoma Jiji imeshinda minne, huku mitatu ikiishia kwa sare.
Kwa takwimu hizo, mchezo huu vita nyingine ya aina yake, huku Dodoma Jiji ikitaka kuendeleza kasi yake na Namungo ikisaka njia ya kurejea kwenye ushindi.