Prime
Murtaza Mangungu amenikumbusha ‘mwaka 1947’
Muktasari:
- Jana, alikusanya kundi akaenda katika uwanja wa mazoezi kule Bunju na kutangaza orodha yake ya wadhamini wa klabu. Orodha ambayo baadaye ilikuja kupingwa na mwenyekiti wa bodi, Crescentius Magori. Mambo fulani hivi ya ovyo ovyo.
RAFIKI yangu Murtaza Mangungu amenikumbusha mbali sana. Mwaka 1947. Usemi wa kawaida kabisa kwa sisi ambao tulikuwa tunasikiliza redio ya taifa zamani. Ndiyo, amenikumbusha mbali sana.
Jana, alikusanya kundi akaenda katika uwanja wa mazoezi kule Bunju na kutangaza orodha yake ya wadhamini wa klabu. Orodha ambayo baadaye ilikuja kupingwa na mwenyekiti wa bodi, Crescentius Magori. Mambo fulani hivi ya ovyo ovyo.
Simba wana ofisi zao nzuri tu pale mjini, lakini Mangungu akaenda kujificha Bunju. Alijua kwamba jambo alilokuwa anafanya ni jambo la kisela zaidi. Alijua kwamba asingeweza kufanyia katika ofisi za Simba kwa sababu angefukuzwa.
Hapo hapo unajiuliza, hivi wale wanachama aliwatoa wapi? Aliwakusanya vipi? Mbona aliwakusanya kimafia vile bila kuwepo kwa tangazo lolote la mkutano. Anajua mwenyewe. Haya mambo yalikuwa yanafanyika mwaka 1947 katika mpira wetu. Umafia.
Lakini akaamua kutangaza orodha ya wadhamini wake huku kurasa rasmi za mitandao ya kijamii za klabu hiyo zikiwa hazina habari. Siku hizi tumezoweshwa kuona mambo rasmi ya klabu yakitangazwa katika kurasa za klabu hizi. Sio timu kubwa tu. Hata timu ndogo kama Mashujaa huwa zinatangaza mambo yao kupitia kurasa rasmi za kijamii kama vile Instagram. Badala yake tangazo la Magori la kutotambua kikao cha Mangungu na wadhamini wake wapya ndilo ambacho tuliliona katika ukurasa rasmi wa Instagram wa Simba. Na hapo ndipo ikawa rasmi kwamba Simba kuna mgogoro mzito.
Tupo mwaka 2026 lakini kina Mangungu wamefanya mambo ya mwaka 1947. Sitaki kujua nani yupo sahihi au nani hayupo sahihi, lakini tunaishi katika dunia ya uwazi sana. Timu kubwa kama Simba ilipaswa iwe imeachana na mambo haya zamani. Kwamba wakubwa hawawasiliani katika mambo nyeti kama kuchagua bodi ya wadhamini?
Mangungu yupo upande wa wanachama lakini ana namba ya simu ya Magori. Mangungu anajua ofisi za Simba zilipo. Hata kama kuna upande wa mwekezaji kilishindikana nini kuwepo kwa mawasiliano baina ya pande mbili kabla kwenda Bunju?
Uteuzi wa mmoja kati ya wale ambao Mangungu amewateua unatia shaka. Rafiki yetu Salim Abdallah Muhene ‘Try Again’ naye jina lake limechomoza katika orodha ya watu wa Mangungu. Inadaiwa kwamba Try Again hayupo sawa na uongozi wa sasa wa Simba.
Kwamba hakuridhishwa na maamuzi ya tajiri wa timu, Mohamed Dewji na kuondolewa katika nafasi ya mwenyekiti wa bodi. Inadaiwa kwamba ameingia msituni. Na kwa jina lake kujitokeza katika orodha ya Mangungu imekuwa kama vile kuthibitisha kwamba ameibukia katika kambi ya upande wa wanachama wenye asilimia 51 ya hisa klabuni baada ya muda mrefu kuwa katika upande wa tajiri wenye hisa 49.
Maisha ya Simba ya leo hayaeleweki. Wakati Try Again akiwa mwenyekiti wa bodi alikuwa anasemwa na watu mbalimbali kwamba yeye ndiye aliyekuwa tatizo klabuni kwa sababu aliua mawasiliano ya watu wengi na tajiri.
Tajiri amemuweka kando na inaonekana kama ameibukia upande wa pili. Simba kuna moto unawaka. Zamani mambo haya yalikuwepo lakini katika dunia mpya ya mpira wa kisasa ni mambo yaliyopitwa na wakati. Ukiona mambo hayaendi kama unavyotaka unaamua tu kuachana na timu. Hata hivyo watu wa Simba wameamua kutunishiana misuli.
Kule kwa mtani maisha yao ni shwari. Watu wamekubaliana na hali ya kwamba wana tajiri mmoja, na tajiri ana mtu wake anayeitwa Hersi Said ambaye ana genge la vijana wenzake wanaoendesha timu.
Watu wengi maarufu wa zamani wa Yanga wameamua kukaa kando na kushangilia mabao ya kina Maxi Nzingeli. Walikuwepo kina Seif Magari lakini sasa hivi wameamua kukaa kando kupisha utawala wa GSM na watu wake.
Simba watu wakiwekwa kando huwa wanaingia msituni. Hii ndio tofauti ya Simba na Yanga. Usidhani kama Mangungu yuko peke yake katika vita hii. Lazima ana watu wazito nyuma yake ambao wanasukuma jambo. Na kuna kinachodaiwa kwamba wapo watu wazito ambao hawamtaki tajiri.
Yote haya yanatokea wakati Simba ikiwa katika usajili wa wachezaji. Wanaandaa timu yao kwa ajili ya msimu ujao. Wanataka kukomesha utawala wa Yanga ambako mambo ni shwari.
Yanga imechukua ubingwa mara tano mfululizo. Simba wamejiliwaza kwa kutwaa ubingwa wa Shirikisho, lakini ukweli ni kwamba lengo lao kuu ni kuupora ubingwa wa Ligi Kuu. Hili ndilo kombe la msingi nchini. Hata hivyo, kabla hawajatia mguu katika msimu ujao tayari wameshaanza kuvurugana. Tarehe 12 wana mechi dhidi ya Peter Shalulile pale Uwanja wa New Amaan lakini tayari wameanza kuvurugana.
Hiki alichofanya Mangungu kimenikumbusha mbali. Mwaka 1947 wakati huo upande fulani wa wanachama wenye mgogoro katika klabu yao wakiiteka timu kutoka nyumba ya kulala wageni na kuipeleka kusikojulikana.
Usiku wa manane kuna watu wazito wangeenda na basi lao chakavu katika nyumba ya kulala wageni ya aliyekuwa mwenyekiti wao, Yusuf Hazali na kuwateka wachezaji. Baadaye mwenyekiti akiamka asubuhi anajikuta hajui timu ilipo. Kumbe imepelekwa katika Hoteli ya Njuweni pale Kibaha. Sijui jambo hili la Mangungu litaishia wapi, lakini sioni akishinda hii vita. Siku hizi mpira umekuwa pesa. Mashabiki na viongozi wengi watakuwa upande wa tajiri na Mangungu ataonekana mvurugaji wa mambo tu.
Fikiria namna ambavyo rafiki yetu Swedi Mkwabi wala hakuwa na jambo baya pale Simba, lakini watu wakamtengenezea zengwe kwa tajiri akalazimishwa kujiuzulu.
Sembuse Mangungu ambaye ametoa mapanga hadharani? Tajiri akisusa tu basi Mangungu kazi anayo. Sijui amejiandaa vipi na hii vita lakini ana kazi ngumu. Tajiri akienda hadharani tu kudai kwamba hatasaini tena wachezaji wala kulipia kambi basi kazi ipo. Yatarushwa mawe mengi kutoka kila upande kwenda kwa mzee wetu wa Kilwa.