Prime
Makocha wengi wakionyesha mapenzi tutalinda soka letu?
PEP Guardiola ni mpenzi mkubwa wa Barcelona, klabu aliyoichezea kwa kipindi kirefu na kwa mafanikio kabla ya kuingia katika kazi ya ukocha ambayo pia aliifanya katika timu hiyo kutoka Jimbo la Catalonia, Hispania.
Ukweli kwamba makao makuu ya Barcelona yako Catalonia unamfanya mtu kama Guardiola kuwa na mapenzi ya dhati kwa klabu hiyo kutokana na siasa za Hispania ambazo kwa muda mrefu zimejikita katika mzozo wa jimbo hilo kutaka kujitoa chini ya utawala wa nchi hiyo.
Ndiyo maana, kila kunapokuwa na maamuzi muhimu yanayohusu siasa hizo, Guardiola hukimbia haraka kurejea Hispania kushiriki. Mfano ni pale alipolazimika kusafiri kutoka Ujerumani kwenda kupiga kura ya maoni kuhusu kujitenga kwa Catalonia na Hispania.
Kwa hiyo, huhitaji kumsubiri Guardiola akuambie kwamba anaipenda Barcelona. Historia yake na msimamo wake kuhusu siasa za Hispania vinafahamika wazi. Lakini, jambo hilo halijawahi kuwafanya watu waamini kwamba anaweza kukiuka maadili ya kazi anapoiongoza klabu nyingine kucheza dhidi ya Barcelona.
Hakuna anayetarajia apange kikosi kibovu ili timu yake ipoteze kwa makusudi dhidi ya klabu anayoipenda. Uadilifu hutawala uamuzi wake, na ikipewa kichapo, basi iwe kwa uwezo wa mpinzani.
Mfano mzuri ulitokea mwaka 2015 alipokuwa kocha wa Bayern Munich, mwaka mmoja baada ya kuondoka Barcelona. Katika nusu fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya timu hizo zilipokutana mchezo wa kwanza ulipigwa Barcelona.
Barcelona ikiwa na safu kali ya ushambuliaji iliyoundwa na Luis Suarez, Neymar na Lionel Messi ilihangaishwa katika kipindi cha kwanza kabla ya Messi kufunga mabao mawili na kuiongoza timu hiyo kushinda mabao 3-0.
Katika mchezo wa marudiano jijini Munich, Bayern, ambayo iliwakosa Franck Ribery, David Alaba na Arjen Robben mchezo wa kwanza, ilishinda mabao 3-2 lakini ikaaga mashindano kwa jumla ya mabao 5-3.
Mjadala baada ya mchezo huo haukuwa kwamba Guardiola alifanya njama ili Barcelona ishinde, ingawa alifanya mabadiliko ya kimfumo ambayo pengine yaliipa nafasi safu ya Neymar, Suarez na Messi, ambayo hadi wakati huo ilikuwa tayari imefunga zaidi ya mabao 100 kuondoka na ushindi mkubwa.
Watu walizungumzia jinsi Guardiola alivyoweka mkakati wa kuwabana nyota hao watatu na namna viungo kama Xabi Alonso, Bastian Schweinsteiger na Philipp Lahm walivyojaribu kudhibiti eneo la kiungo huku karibu timu nzima ikicheza mtu kwa mtu.
Wachambuzi kama Jamie Carragher walishangazwa na mkakati wa Guardiola kuanza mchezo akiwa na mabeki watatu kabla ya baadaye kubadili mfumo na kutumia mabeki wanne. Hakuna aliyenusa harufu ya upangaji matokeo.
Mtazamo huo hauwezi kufanana na ule wa kocha na mchezaji wa zamani wa Simba, Jamhuri “Julio” Kihwelo, ambaye amekuwa gumzo wiki hii baada ya kuibuka katika mkutano wa wanachama wa tawi na kuelezea jinsi mapenzi yake makubwa kwa Simba yanavyomsukuma hadi kuthubutu kukiuka maadili ya kazi.
Imekuwa ni kawaida kumsikia Kihwelo akizungumzia Simba kama klabu anayoipenda na ambayo aliitumikia hata ilipokuwa inapitia matatizo ya kifedha, huku akitekeleza majukumu yake kwa umakini. Hilo halina tatizo, kwa sababu kama mchezaji wa zamani wa Simba ni jambo la kawaida kuwa na mapenzi ya kiwango hicho.
Isitoshe, taifa limegawanyika katika makundi mawili kutokana na ukubwa na historia ya Simba na Yanga. Kwa hiyo, mtu yeyote anayependa mpira wa miguu mara nyingi huwa na mapenzi na moja ya klabu hizo.
Lakini, Kihwelo amekwenda mbali zaidi ya mapenzi na ushabiki. Katika mkutano huo wa tawi, aliwaambia wanachama kuwa amekuwa akidiriki kufanya kila awezalo ili Simba ipate ushindi, akitoa mfano wa jinsi alivyosababisha penalti wakati Simba ilipocheza na Kajumulo pamoja na kudai kufanya hivyo hata katika baadhi ya mechi.
Hapo ndipo mipaka ya maadili inapovukwa na hadhi ya Ligi Kuu inaanza kuathirika, wakati ligi hiyo imeanza kuvutia nyota kutoka sehemu mbalimbali za Afrika na nje ya bara hilo.
Kati ka nc hi zil izoendelea kimichezo, kukiri kufanya makosa ya aina hiyo kunaweza kusababisha uchunguzi wa kina na hata adhabu kali kwa aliyetoa kauli hiyo. Sababu ni kwamba, kwa kujua mapenzi yake kwa klabu fulani, mtu anaweza kupelekwa kufundisha timu nyingine kwa mkakati maalumu unaolenga kuathiri mwenendo wa ligi. Nani anajua?
Na kama uchunguzi ukibaini madai hayo ni ya kweli, adhabu inaweza kumkumba kocha husika au hata timu iliyohusika katika njama hizo, iwe alifanya hivyo kwa hiari au kwa ushawishi wa watu wengine. Lakini nani atafuatilia jambo hilo na kuchukua hatua zinazostahili?
Kinachoweza kusukuma uchunguzi ni kauli yake mwenyewe kwamba alifanya vitendo hivyo. Hatujui mamlaka zinazohusika zinalichukuliaje suala hilo.
Kwa mamlaka zinazowajibika, tayari zingekuwa zimetoa tamko kuhusu tukio hilo na kueleza kuwa hatua zaidi zinafuata. Lakini, mamlaka ambazo kwanza huangalia huyu ni chawa au si chawa, haziwezi kuchukua hatua yoyote.
Badala yake, huenda zikatoa maelezo mengi ya kuhalalisha kilichotokea na kudai hakuna sheria iliyokiukwa. Je, hata Chama cha Makocha Tanzania (TAFCA) hakijaona tatizo la kimaadili kwa mwenzao? Hakijaona kuwa taaluma yao imejeruhiwa? Au nacho kinamsubiri kiongozi mkuu wa soka atoe kauli ndipo nacho kifungue mdomo?
Kitendo hicho kimeonyesha kwamba kuna shida kubwa zaidi. Bila kuanza kuushughulikia mapema shida iliyopo, wale wenye mapenzi na klabu nyingine nao wanaweza kuanza kuiga.
Kumbuka, timu nyingi zinazofundishwa na makocha wazawa zinaongozwa na watu ambao ama ni mashabiki au waliwahi kuzichezea klabu hizo.
Fred Felix Minziro ni Yanga kindakindaki na aliichezea kwa kujituma hadi alipoondoka. Juma Mgunda ni Coastal Union damdam, na maisha yake yote ya soka yamefungamana na klabu hiyo. Juma Kaseja ni mmoja wa magwiji wa Simba. Je, nao wakianza kuonyesha hivyo mpira wetu utakuwa salama?