Hello

Your subscription is almost coming to an end. Don’t miss out on the great content on Nation.Africa

Ready to continue your informative journey with us?

Hello

Your premium access has ended, but the best of Nation.Africa is still within reach. Renew now to unlock exclusive stories and in-depth features.

Reclaim your full access. Click below to renew.

MAUAJI YA KUTISHA -04

Muktasari:

  • “Mke wangu nakuomba ujikaze, kuna tukio limetokea hapa Mikocheni.”

ALIPONITHIBITISHA kuwa kweli mwanawe alikuwa ameuawa akaenda pembeni na kumpigia simu mke wake.

“Mke wangu nakuomba ujikaze, kuna tukio limetokea hapa Mikocheni.”

“Tukio gani?” Mke wake akamuuliza kwenye simu.

“Martin ameuawa!”

“Martin ameuawa?”

“Ndiyo.”

“Martin yupi?”

“Martin mtoto wetu.”

“Usiniambie! Martin ameuawa wapi?”

Almasi akamueleza kama alivyoelezwa na polisi.

“Ninakuja huko huko.”

“Usije. Mwili wake utaondolewa sasa hivi. Tafadhali subiri hapo hapo nyumbani. Nitakuwa ninakufahamisha kila kitu.”

Almasi akakata simu.

Hapo ndipo kachero Inspekta  Amour alipowasili. Baada ya Amour kupata maelezio kutoka kwa polisi aliowakuta hapo alitambulishwa kwa mzee Almasi ambaye alimwambia alimuhitaji ofisini kwake watakapoondoka hapo.

Nusu saa baadaye mwili wa Martin ulipakiwa kwenye gari la  polisi na kupelekwa hospitali ya Muhimbili. Polisi nao waliondoka wakiwa na mashuhuda watatu ambao walikwenda nao  kituo  cha polisi kuandikisha maelezo.

Inspekta Amour naye alirudi ofisini kwake.

Nusu saa tu baadaye, Almasi aliyekuwa bado akitokwa na machozi  alibisha ofisini humo.

Amour alimkaribisha, Almasi aliingia na kuketi kwenye kiti.

“Mzee uliniambia kuwa yule ni mwanao.”

“Ndiyo ni mwanangu” Almasi alimjibu kabla ya kujifuta uso wake kwa kitambaa.

“Ni mwanao  wa  ngapi?”

“Ni mwanangu wa  kwanza.”

“Anaitwa nani?”

“Anaitwa Martin Almasi.”

“Alikuwa anatoka wapi na alikuwa anakwenda wapi kabla ya kukutwa na tukio lile?”

“Nadhani alikuwa anatoka  benki. Nilikuwa nimemtuma aende benkii akachukue mishahara ya  wafanyakazi wetu  wa  kiwanda cha maji safi ambacho kipo  pale pale Mikocheni.”

“Kwa hiyo lile tukio limemkuta wakati anatoka  benki?”

“Nafikiri  ni hivyo.”

“Hakukuwa na fedha zilizokutwa kwenye gari, huenda fedha  hizo zimeporwa. Unadhani  alikuwa amechukua kiasi gani kutoka benki?”

“Tulipanga kwamba angechukua shilingi milioni themanini”

“Kama kweli atakuwa amechukua pesa hizo ni kwamba shilingi milioni themanini zitakuwa zimeporwa?”

“Itakuwa ndiyo hivyo.”

“Walioshuhudia tukio hilo wameeleza kwamba waliona watu watatu ambao waliisimamisha  gari yake kisha wakamfuata kwenye mlango  ambapo mmoja alitoa panga na kumchinja  na  kisha kuchukua mkoba wake ambao unadhaniwa ndio uliokuwa na pesa…”

Almasi alliijifuta  machozi kabla ya kumtazama tena Inspekta Amour.

“Kwa hiyo hilo litakuwa ni tukio  la ujambazi?”

“Kwa vile kuna pesa ambazo zimeporwa litakuwa ni tukio la ujambazi lakini kinachotutatiza ni hao  watu walioonekana wakifanya ujambazi huo. Hawakuwa watu wa  kawaida.”

“Walikuwaje?”

“Inasemekana walikuwa watu watatu. Wawili walikuwa wamevaa mavazi meupe, mmoja alivaa mavazi meusi. Huyo aliyekuwa amevaa mavazi meusi kichwa chake kilikuwa kimechinjwa na kilikuwa kinaning’inia.”

Uso wa Almasi ulionesha mshangao.

“Kichwa chake kilikuwa kimechinjwa na nani?” Akauliza.

“Ndiyo haifahamiki. Sasa huyo ambaye ameelezwa kwamba kichwa chake kilikuwa kinaning’inia ndiye aliyemchinja marehemu na kupora mkoba wake wa fedha.”

“Sijakuelewa Inspekta.  Mtu huyo angewezaje kumchinja mtu wakati yeye mwenyewe alikuwa amechinjwa?”

“Huo ndio utata uliopo katika hili tukio. Hili si tukio la  kawaida ndiyo maana limeishitua serikali.”

“Si la kawaida kweli. Sijawahi kuona majambazi wa aina hiyo!”

“Na hata  mimi pamoja  na kufanya kazi hii kwa karibu robo tatu ya umri wangu, sijawahi kuona majambazi wa aina hiyo.  Kinachokushangaza wewe ndicho kinachonishangaza mimi.”

“Kumbe mwanangu aliuawa na watu hao?”

“Watu hao ndio waliomuua mwanao.”

“Sasa baada ya kupora huo mkoba wa fedha walitoweka vipi?”

“Haifahamiki. Watu  walioshuhudia  tukio hilo wamesema hawajui jinsi watu hao walivyotoweka.”

“Mmh…! Hilo tukio ni la kushangaza sana.”

“Sasa sisi tunaendelea na uchunguzi wetu. Mkurugenzi wa upelelezi amenipa jukumu la kuwasaka watu hao ili wapatikane na kufikishwa kwenye vyombo vya sheria.”

“Sasa huyo anayedaiwa kuwa amechinjwa kisha akamchinja Martin atakuwa yuko hai kweli?”

“Maswali mengi tutakuwa tunajiuliza kwa sasa lakini hayatakuwa na  majibu. Majibu yatapatikana wakati uchunguzi wetu utakapokamilika. Lakini kama mtu  huyo alikuwa hai wakati akifanya tukio hilo, atakuwa hai hadi hivi sasa.”

“Mimi nawaomba muwasake hao watu ili tuwajue ni kina nani na pia washughulikiwe kwa mujibu wa sheria.”

“Tuko pamoja.”

Baada ya hapo Inspekta Amour alichukua namba ya simu ya  Almasi. Alimwambia atakapomhitaji tena atampigia.

Allmasi alipoondoka ofisini humo, Inspekta Amour aliinua mkono wa simu iliyokuwa mezani kwake.

Alibonyeza tarakimu. Simu  ya upande wa pili ilipopokelewa alisema.

“Inspekta Amour hapa. Ninawataka wale mashuhuda  wa tukio la mauaji na ujambazi lilitokea kule Mikocheni.”

“Unawahitaji wafikishwe huko makao makuu?” Sauti ikauliza kutoka simu ya upande wa pili.

“Ndiyo.  Ninawahitaji  ofisini kwangu kwa mahojiano.”

“Sawa.”

Amour akaurudisha mkono wa simu.

Kama kawaida yake aliinuka na kwenda kusimama kando ya dirisha.

Kwa mara nyingine tena alijiuliza kama mashuhuda wa tukio hilo  walimuona sawa sawa mtu aliyemchinja Martin. Alijiuliza hivyo baada ya kuona kuwa ilikuwa haiwezekani kwa mtu ambaye  shingo yake ilikuwa imechinjwa aweze kumchinja  mtu mwingine.

Kama kulikuwa na utata  katika  tukio hilo,  Amour alijiambia, utata ulikuwa ni huo.

Alijaribu kulifananisha tukio hilo na tukio ambalo  lilitokea zamani ambapo mwanamke mmoja aliuawa na uchunguzi ulikuja kuonesha kuwa mtu aliyemuua alikuwa ameshakufa mwaka mmoja uliopita.

Mashuhuda wa tukio hilo waling’ang’ania kueleza kuwa aliyemuua mwanamke huyo alikuwa Christian Bambo wakati taarifa zilizopo Bambo alishakufa kabla ya tukio hilo.

Bambo alikutwa ameungua na  kuteketea kwa moto baada ya gari lake kuwaka  moto huku mwenyewe akiwemo ndani.

Lakini mwaka mmoja baadaye Bambo huyo  huyo alikuja kuonekana na watu akimuua mjane wake kwa kumpiga risasi na hatimaye  kutoweka.

Alama za vidole zilizokutwa katika eneo la  tukio zilikuwa  ni za Bambo lakini Bambo mwenyewe alishathibitika kuuawa kwa moto huku mke wake akithibitishia polisi kuwa gari la mume wake lilikuwa na matatizo yaliyosababisha lilipuke na  kuwaka  moto uliomteketeza  mwanaume huyo.

Baada ya uchunguzi wa mwaka mzima, Amor alikuja kugundua mbinu zilizotumika kumficha muuaji. Bambo alikuja kukamatwa jijini Nairobi akiwa hai.

Uchunguzi ulionesha kuwa hakuwa ameteketea kwa moto na kufa bali aliyeteketezwa alikuwa mtu mwinggine lakini aliwekewa vitambulisho vya Bambo mfukoni mwake.  Hivyo mwili wake ulioungua ulipopekuliwa ulikutwa na mabaki ya vitambulisho vya  Bambo. Polisi wakaamini kuwa aliyeteketea alikuwa Bambo.

Mke wake ambaye alikula  njama  na mume wake alilipwa bima na alirithi mali za Bambo lakini Bambo akiwa mafichoni alikuja kukorofishana na mke wake kuhsu mali, ndipo alipoamua kumuua jambo ambalo lilizua utata wa nani aliyemuua.

Kumbe yule mtu aliyeteketezwa na moto alikuwa ni ndugu yake Bambo. Bambo alimteketeza ndugu yake ili  achukue mali yake kwa vile hakuwa na mke wala watoto.

Alivyokufa  haikujulikana kwamba alikufa  yeye. Watu hawakujua alikuwa amekwenda  wapi. Badala  yake walijua kuwa aliyekufa alikuwa Bambo.

Hatimaye Bambo alikamatwa na kuhukumiwa kunyongwa.

Amour alijiambia muuaji wa Martin anaweza kuwa kama Bambo.

Nusu saa tu baadaye polisi  mmoja alibisha ofisini mwa Inspekta amour na alipokaribishwa alimwambia Amour kuwa amekuja na mashuhuda wa tukio la mauaji ya Mikocheni.

“Wako wangapi?” Amor alimuuliza.

“Ni watatu.”

“Wambie waingie mmoja  mmoja. Nataka kuwahoji maswali.”

Polisi  huyo alitoka.  Baada ya dakika moja aliingia na mtu mmoja.

“Mtu wa kwanza ni huyu Afande,” alimwambia Amour kisha akatoka ofisini.

“Kaa kwenye kiti.” Amour alimwambia  mtu huyo.

Alikuwa kijana wa umri  usiopungua miaka  ishirini  na minane. Jinsi alivyonyoa nywele zake, sura yake na mavazi yake, alionesha alikuwa ni mmoja wa vijana wa mjini wanaopenda kushinda vijiweni wakisubiri wasichana  wapite wawatongoze.

Kijana huyo alikaa kwenye kiti kwa taratibu kama vile aliogopa kukivunja.

Ofisi ya polisi ni ya polisi tu. Unapoingia hata kama huna kosa ni lazima unywee.

“Jina lako tafadhali.” Amour alimuulliza akiwa ameshika  kalamu.

“Naitwa Shefa Ibrahim.”

Amour aliandika jina lake kabla  ya kumuuliza.

“Una umri  gani?”

“Mwezi ujao  nitatimiza miaka ishirini na tisa.”