Bodi ya filamu yamfungia Mwanaharusi kwa miezi sita
Muktasari:
- Uamuzi huo umetolewa baada ya Bodi kufanya kikao cha maadili na Mwanaharusi, kufuatia tukio la ukiukwaji wa maadili lililotokea wakati wa maandalizi ya utayarishaji wa filamu katika eneo la Chanika, Dar es Salaam.
Bodi ya Filamu Tanzania imemfungia Bi. Mwanaharusi Ally Makwinjo kufanya shughuli za filamu na michezo ya kuigiza kwa kipindi cha miezi sita, kuanzia Septemba 15, 2026.
Uamuzi huo umetolewa baada ya Bodi kufanya kikao cha maadili na Mwanaharusi, kufuatia tukio la ukiukwaji wa maadili lililotokea wakati wa maandalizi ya utayarishaji wa filamu katika eneo la Chanika, Dar es Salaam.
Bodi imeeleza kuwa baada ya kupitia na kujadili suala hilo kwa kina, imeona hatua hiyo inastahili kuchukuliwa kutokana na kosa la kimaadili lililohusishwa na tukio hilo.
Aidha, Bodi imeendelea na uchunguzi wa kuwafuatilia wahusika wengine waliohusika katika tukio hilo, huku ikisisitiza kuwa hatua stahiki zitachukuliwa kwa mujibu wa taratibu zinazosimamia tasnia ya filamu na michezo ya kuigiza nchini.
Bodi ya Filamu imeongeza kuwa itaendelea kuchukua hatua pale itakapobaini mdau yeyote wa tasnia amekiuka maadili.