Fei Toto aumiza kichwa kurudi kikosini Yanga

Muktasari:

Kiungo huyo msimu uliopita alikuwa mchezaji tegemeo katika eneo la kiungo cha Yanga na kuisaidia timu hiyo kumaliza nafasi ya pili katika Ligi Kuu Bara.

Dar es Salaam. Kiungo wa Yanga, Feisal Salum amesema kukosa kwake nafasi ya kucheza kikosi cha kwanza katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa dhidi ya Township Rollers kunamfanya ajitathimini ni wapi anakosea.

Yanga iliambulia sare ya bao 1-1 dhidi ya Township Rollers kwenye uwanja wa nyumbani na wanatarajia kuwafuata wapinzani wao kwaajili ya mchezo wa marudiano unaotarajiwa kuchezwa kati ya Agosti 20 hadi 23.

Fei Toto alisema nafasi yake katika kikosi cha kwanza inachangamoto kubwa kutokana na usajili uliofanyika kila mchezaji anatakiwa kupambana mwenyewe kuhakikisha anajitengenezea mazingira ya kupata namba kikosi cha kwanza.

"Nimeona makosa kidogo kwa wenzangu na hiyo ndio itakayokuwa njia ya mimi kuyafanyia kazi na kuonyesha mazoezini ili niweze kurudi kikosini na naamini hilo linawezekana."

"Kuona mapungufu yao haina maana kwamba hawakucheza inavyotakiwa walicheza vizuri, lakini kuna vitu walitakiwa kuviongeza ili timu iweze kupata matokeo hivyo nimeshaanza kuvifanyia kazi ili niweze kupata nafasi ya kucheza mchezo wa marudiano," alisema Fei Toto.