Aussems aliisoma Nkana zamani Simba msiwe na shaka!

Muktasari:

Simba imefanikiwa kutinga kucheza mechi za raundi ya kwanza na Nkana baada ya kuing'oa Mbabane Swallows ya Eswatini kwa jumla ya mabao 8-1, nyumbani 4-1 na ugenini 4-0.

Dar es Salaam. Kocha Mkuu wa Simba, Mbelgiji Patrick Aussems amewaambia mashabiki na wanachama wa klabu hiyo wasiwe na wasiwasi kabisa juu ya Nkana ya Zambia watakayokutana nayo katika Ligi ya Mabingwa Afrika.

Aussems ambaye kikosi chake kimefuzu hatua ya awali ya mashindano hayo na sasa watacheza na Nkana mechi ya raundi ya kwanza na mchezo wa kwanza utapigwa nchini Zambia kati ya Desemba 13-14 na wa marudiano utakuwa Desemba 23-24.

Amesema, watatumia kipindi cha wiki moja kufanya maandalizi juu ya mchezo huo na kwa sababu ameshajua wapinzani wao ni wa aina gani haiwasumbui.

"Tunakwenda kujiandaa kwa ajili ya mchezo huo na kikubwa ni kwamba tuna timu nzuri ya kucheza mashindano hayo kwa nguvu na kufanya vizuri bila wasiwasi,"alisema Aussems aliyesisitiza kwa sasa kikosi chake hakina majeruhi hata mmoja.

Amesema, haina ubishi kama ilivyotokea Eswatini na kwa timu hiyo ya Zambia itakuwa hivyo: "Nilianza kuzifuatilia zamani hizo timu ambazo tulitarajia kukutana nazo hivyo Nkana pia ilikuwa miongoni mwao kilichobaki ni kazi tu."

Akizungumzia kwa namna gani alivyopokea kuanza mechi yao ugenini na ya marudiano nyumbani: "Kwetu ni vizuri ingawa ni mpango wa ratiba ilivyo, tulianza kucheza nyumbani na Mbabane na sasa tunaanzia ugenini kwa Nkana."