Yanga yaichapa Geita, Mzize akirejea
Muktasari:
- Ushindi huo unaifanya Yanga kufikisha pointi 18, ikishinda mechi sita mfululizo.
Yanga imeendeleza moto wake kwenye Ligi Kuu Bara baada ya kuichapa Geita Gold kwa bao 1-0 ikiendelea kuongoza msimamo wa ligi.
Ushindi huo unaifanya Yanga kufikisha pointi 18, ikishinda mechi sita mfululizo.
Yanga imelazimika kucheza pungufu kwa dakika 72 na kutengeneza ushindi huo kwa bao pekee lililofungwa dakika ya 54 ya kipindi cha pili na beki Farouk Koumara kwa kichwa akitumia kona ya Maxi Nzengeli.
Mapema dakika 18 Yanga imepata pigo baada ya kiungo Stephanie Aziz KI kuonyesha kadi nyekundu ya moja kwa moja baada ya kumchezea vibaya beki Datius Peter.
Awali, mwamuzi Abdisalim Wajih alimuonyesha kiungo huyo kadi ya njano, lakini alipokwenda kujiridhisha kupitia marudio ya video akabadili uamuzi na kumpa kadi nyekundu Aziz KI.
Yanga licha ya kadi hiyo imeishambulia Geita ikitawala kipindi cha kwanza ambapo nafasi bora dakika ya 34 mshambuliaji wake Seleman Mwalimu amewatoka mabeki wa Geita huku kipa akiwa amelala chini akashindwa kufunga.
Geita ikaikalia kooni Yanga dakika 10 za mwisho kuanzia dakika ya 85 na zile tano za nyongeza ikawashambulia wenyeji, lakini hata hivyo haikupata bao.
Kiungo wa Geita Golda, Abdul Ameir ameshindwa kufunga kwa shuti kali lililogonga mwamba na kurudi uwanjani.
Mpaka mwisho wa mchezo Yanga imefanikiwa kutoka na ushindi wa bao 1-0 huku Geita ikiendelea kuwa mteja kwa abingwa ha watetezi, ikipoteza mechi ya saba kiujumla baina ya timu hizo.
Tukio lingine zuri kwa mashabiki wa Yanga ni kurejea kwa mshambuliaji wake Clement Mzize aliyeingia dakika ya 65 akichukua nafasi ya Mwalimu.
Mzize amecheza mechi yake ya kwanza baada ya kuwa nje tangu msimu uliopita baada ya kuumia goti na kufanyiwa upasuaji