Josiah atuma ujumbe Ligi Kuu
Muktasari:
- Mashujaa mpaka sasa imecheza mechi nne za ligi, ikipoteza mbili mfululizo ugenini dhidi ya Fountain Gate (1-0) na Mbeya City (2-1), ilianza kwa kuifunga Coastal Union (1-0) ugenini, kisha ushindi wa 2-1 nyumbani mbele ya Kagera Sugar.
BAADA ya ushindi wa kwanza kwenye uwanja wa nyumbani ikitoka kupoteza mbili mfululizo ugenini, kocha wa Mashujaa, Amani Josiah amesema matokeo hayo yamewapa nguvu na kujiamini zaidi hasa wanapokuwa nyumbani.
Mashujaa mpaka sasa imecheza mechi nne za ligi, ikipoteza mbili mfululizo ugenini dhidi ya Fountain Gate (1-0) na Mbeya City (2-1), ilianza kwa kuifunga Coastal Union (1-0) ugenini, kisha ushindi wa 2-1 nyumbani mbele ya Kagera Sugar.
Akizungumza na Mwanaspoti, kocha Josiah amesema tulijua haitakuwa rahisi kwa sababu wapinzani wetu walikuwa wametoka kupoteza ugenini, hivyo walikuja wakiwa na nia ya kubadilisha matokeo yao. Lakini wachezaji wangu walionesha tabia nzuri ya kupambana.”
Kocha huyo amesema kwa sasa wanachotakiwa ni kuhakikisha wanatumia matokeo hayo kama msingi wa kujenga mwendelezo mzuri katika michezo inayofuata, huku akisisitiza umuhimu wa ushindi huo katika kuongeza hali ya kujiamini ndani ya kikosi.
“Tunataka kutumia matokeo haya kutuweka vizuri zaidi. Ushindi kama huu unaongeza kujiamini, lakini tunatakiwa kuutumia kama mwanzo wa kujenga mambo mazuri zaidi kwenye mechi zinazofuata,” amesema.
Kocha Josiah aliwapongeza wachezaji akisema “pongezi kwa wachezaji wangu kwa sababu walikuwa imara. Tulikuwa nyuma, lakini hawakukubali kuwa wanyonge. Waliendelea kupambana, wakatengeneza nafasi na hatimaye tukapata ushindi.”
Mashujaa itarejea tena ugenini kwenye mechi ya tano ya ligi ambapo itakutana na Dodoma Jiji, Septemba 4, 2026 Saa 1:00 usiku kwenye Uwanja wa Jamhuri, Dodoma.