Saa 24 za Ngoma Yanga

Muktasari:

>> Mshambuliaji huyo Mzimbabwe tangu kuanza msimu huu amekuwa akisumbuliwa na majeruhi ya mara kwa mara

Dar es Salaam. Mshambuliaji wa Yanga, Donald Ngoma amebakiza saa 24 kuendelea kuwa mchezaji wa mabingwa hao wa Ligi Kuu Bara..

Taarifa za kutoka ndani ya uongozi wa Yanga zinasema klabu hiyo ilitoa muda maalum kwa Ngoma aliyetimkia kwao Zimbabwe endapo atashindwa kurejea Dar es Salaam leo saa sita usiku atasimamishwa.

Mbali na kusimamishwa Ngoma endapo atashindwa kuheshimu muda huo kesi yake itapelekwa katika kamati ya nidhamu ya klabu hiyo ambapo uamuzi ya kumtimua kabisa yanaweza kuchukuliwa.

Kocha Mkuu wa Yanga, George Lwandamina amethibitisha mshambuliaji wake huyo amepewa muda wa kuhakikisha anakuja nchini kujieleza kwa utoro wake.

"Nimeambiwa na uongozi kuwa alitakiwa (Ngoma) kuwa nchini Novemba 24 sasa kama hatakuja au atakuja hayo yataamuliwa na uongozi," alisema Lwandamina.