Mwamuzi Sasii kuzihukumu tena Simba, Yanga

Muktasari:

  • Mwamuzi huyo ndiye mwamuzi bora wa msimu uliopita wa Ligi Kuu Bara

Dar es salaam. Mwamuzi Bora wa msimu uliopita, Elly Sasii ndiye aliyeteuliwa kuchezesha pambano la watani wa jadi nchini, Simba na Yanga litakalopigwa Jumamosi hii kwenye Uwanja wa Uhuru.

Kwa mujibu wa chanzo kutoka ndani ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), mwamuzi huyo kijana ndiye atakayepuliza kipyenga katikati ya Uwanja wa Uhuru na kusaidiwa na washika vibendera Joseph Bulali na Sudi Lila, huku mezani akiwa mkongwe, Israel  Nkongo.

Simba na Yanga zinatarajiwa kuvaana katika pambano lao la kwanza la Ligi Kuu Bara msimu huu, linalokuwa la 99 kwa timu hizo kukutana katika ligi tangu mwaka 1965.

Sasii ndiye aliyechezesha pambano la Ngao ya Jamii kati ya Simba na Yanga lililochezwa Agosti 20 kwenye Uwanja wa Taifa na Yanga kulala kwa mikwaju ya penalti 5-4 baada ya dakika 90 za mchezo huo kumalizika kwa suluhu.