Yanga yapewa mchongo kuimaliza Zesco

Muktasari:

  • Mtanzania Elias Maguli anayekipiga Nakambala Leopard ya Zambia, ameichunguza Zesco itakayocheza na Yanga, Septemba 28 kisha akaeleza aina yao uchezaji ili Wanajangwani wasipate shida kupata matokeo.

STRAIKA nyota wa zamani wa Simba anayekipiga kwa sasa Nakambala Leopard ya nchini Zambia, amewapenyezea siri Yanga namna yakuwamudu wapinzani wao Zesco United watakaocheza nao katika mechi ya marudiano ya Ligi ya Mabingwa Afrika.
Yanga na Zesco watarudiana wikiendi ijayo baada ya sare ya 1-1 nyumbani, mechi itakayopigwa Uwanja wa Levy Mwanawasa, Ndola ambapo wawakilishi hao wa Tanzania wanahitaji ushindi au sare ya kuanzia mabao mawili kama inatapa kuingia makundi.
Pamoja na timu yao kuchapwa mabao 3-0 na Zesco, Maguli aliamua kuwa mzalendo wa kuwasoma wapinzani wao ili kuwapa siri Yanga namna ya kushinda mechi hiyo.
Amesema jamaa ni wazuri kwa mashambulizi ya pembeni, wanacheza pasi ndefu na fupi pia wanatumia kaunti ataki na kuwataka Yanga wapate muda wa kuwasoma nyota hatari kwao.
"Mabao tuliofungwa sisi yalikuwa ya mashambulizi ya pembeni katika mchezo na Yanga ninachokifikiria ni Zesco watakuwa wanacheza kaunti ataki ili kuwalazimisha Yanga kufanya makosa"
"Mawinga wao wana kasi na ndio waliotunga kwa namna hiyo, lazima Yanga watulie ili kupata ushindi dhidi ya hawa jamaa,lasivyo wanapaswa kujua kwamba sio wepesi"
"Soka la Zambia lina ushindani wa hali ya juu,yote katika yote naamini Yanga watasonga mbele kwani wao na Azam FC ndio waliobakia kuliwakilisha taifa letu kwenye michuano ya kimataifa"amesema.