Kitambi aachiwa mzigo wa Aussems

Muktasari:

Akizungumza mara ya kumaliza mazoezi jana kwenye viwanja vya Gmykhana jijini Dar es Salaam, Kitambi alisema aliitwa na mtendaji mkuu wa timu hiyo, Senzo Mazingisa na kumwambia kuwa anatakiwa kuandaa programu ya wiki moja na kusimamia vyema.

Dar es Salaam. Wakati Simba ikiwa kwenye harakati ya kusaka nani atarithi mikoba ya Kocha Patrick Aussem, msaidizi wake Denis Kitambi ameendelea na jukumu la kuinoa timu hiyo.

Uongozi wa timu hiyo, utakaa na Aussems siku ya Alhamisi (Novemba 28) ili kuyamaliza na kujua kama wataendelea naye au la, ingawa habari za chini chini zinasema atapewa mkono wa kwa heri.

Ndani ya muda huo msaidizi wa Aussems, Kitambi ndiye atakayekuwa na jukumu la kuendesha programu za mazoezi ya timu hiyo.

Akizungumza mara ya kumaliza mazoezi jana kwenye viwanja vya Gmykhana jijini Dar es Salaam, Kitambi alisema aliitwa na mtendaji mkuu wa timu hiyo, Senzo Mazingisa na kumwambia kuwa anatakiwa kuandaa programu ya wiki moja na kusimamia vyema.

“Majukumu niliopewa ni ya kukinoa kikosi ndani ya wiki moja, hivyo siwezi kuzungumza chochote zaidi ya kufanya nilichoagizwa.

“Uongozi unatarajia kukaa na bosi wangu Aussems Alhamisi, naamini baada ya hapo majibu ya maswali yenu yatapatikana ndio maana sitaki kutabiri nini kitatokea zaidi ya kuvuta subra,” alisema.

Mbali na hilo alizungumzia mazoezi waliofanya jana yalikuwa ya kuwarudisha kwenye utimamu wa mwili baada ya kuwa mapumziko kwa siku mbili.

“Tumeanza mazoezi ya kawaida ya kuwarudisha wachezaji katika hali ya utimamu wa mwili kwa kuwa, walipumzika, si rahisi lakini nimeweza na naamini nitaendelea vyema.

“Programu ninazozifanya ni nje ya bosi wangu Aussems kwani, nimepewa kazi moja kwa moja kutoka kwa mtendaji mkuu, hivyo nimetii maelekezo,” alisema.