Igangula aanza kampeni Yanga kurithi kiti cha Manji

Muktasari:

  • Akizinduzi kampeni hizo, Igangula alisema lengo lake ni kutaka kuhakikisha klabu hiyo inahamia kwenye mfumo wa soka la kisasa ili wawe na nguvu kubwa ya kiuendeshaji.

WAGOMBEA wa nafasi mbalimbali za uchaguzi wa  Yanga SC,  wamezindua rasmi kampeni za kujinadi yale yote ambayo wamepanga kuyafanya kama wakipata nafasi za kuiongoza klabu hiyo.

Uzinduzi huo,  umefanyika leo ukiongozwa na Mbaraka Hussein Igangula kwenye Ukumbi wa Wallace Kata ya 15 CCM uliopo Temeke jijini Dar es Salaam.

Igangula ni mgombea nafasi ya uenyekiti wa klabu hiyo ambayo Mei 20 mwaka juzi,  alijiuzulu  mfanyabiashara maarufu nchini Yussuf Manji.

Akizinduzi kampeni hizo, Igangula alisema lengo lake ni kutaka kuhakikisha klabu hiyo inahamia kwenye mfumo wa soka la kisasa ili wawe na nguvu kubwa ya kiuendeshaji.

"Ndani ya mwaka wangu mmoja nitafanya mabadiliko makubwa ikiwemo maboresho ya jengo letu, pamoja na kuhakikisha Yanga inakuwa na uwanja wake wa kufanyia mazoezi.

"Mfumo wa uwekezaji utarahisisha mambo ndani ya klabu yetu,  lengo ni kutaka Yanga iwe na nguvu kubwa, pia nitakuwa makini na vyanzo vyetu vyote vya mapato, " alisema.

Igangula amekuja na kauli mbiu isemayo Umoja na mshikamano kwa maendeleo ya Yanga.

Mgombea huyo yupo sambamba na makamu wake Titus Ossoro pamoja na wajumbe wa kamati ya utendaji, Silvester Bernard Haule, Benjamini Mwakasonda, Atanas Kazige, Ramadhan Said (Chalinze).