AFCON 2023 rasmi kwenye Startimes
Katika nafasi ya kuonyesha mapinduzi ya eneo la matangazo mubashara ya soka, StarTimes imefanikiwa rasmi kupata haki za kuonyesha mubashara (Live) michuano ya AFCON 2023 nchini Ivory Coast inayoanza Januari 13 hadi Februari 11.
Sambamba na AFCON 2023, Startimes pia imefikia makubaliano na CAF kuonyesha matukio yote ya CAF kwa mwaka 2024 katika nchi za ukanda wa Jangwa la Sahara kwa lugha ya kiingereza na kireno ikiwemo CHAN 2024 na kufuzu AFCON 2025.
Mkurugenzi Masoko na Maudhui Startimes Tanzania, David Malisa amesema mafanikio hayo ni sehemu ya mpango mkakati wa Startimes kuhakikisha watazamaji wanapata maudhui bora ya kimichezo kote Afrika ambako wameendelea kuwa kinara katika hilo.
“Tunayofuraha kutangaza kuwa Startimes imefanikisha kupata haki za matanagzo ya AFCON 2023,” Amesema Malisa
AFCON chini ya CAF ni miongoni mwa matukio bora zaidi ya kimichezo barani Afrika.AFCON 2023 itapigwa nchini Ivory Coast kuanzia Januari 13 na kutamatika Februari 11,2024.Jumla ya mataifa 23 yataungana na mwenyeji kusherehesha AFRIKA na Dunia kwa michezo 52 bora ambayo itaamua nani anakuwa mfalme mpya wa soka la Afrika.
AFCON 2023 ni mwendelezo wa ushirikiano mkubwa wa Startimes na CAF ikikumbukwa AFCON 2019-2022, CHAN 2020 na mashindano ya klabu yaani Ligi ya Mabingwa Afrika na Kombe la Shirikisho Afrika.
“Uwekezaji huu wa Startimes katika AFCON na matukio mengine makuu ya CAF unakoleza thamani ya lengo kuu ambalo ni kuwafikia, kuwaelemisha na kuwaburudisha mamilioni ya watazamaji wake kote Afrika,” amesema Malisa na kuongeza;
“Hili linathibitisha kujizatiti kwetu katika kuwaleta Pamoja na kuwaburudisha mamilioni ya watazamaji wetu kote barani Afrika kupitia maudhui bora toka Tasnia tofauti tofauti, AFCON ni sherehe kubwa ya soka inayokutanisha Afrika yote Pamoja, tunafuraha kuwa sehemu ya kuwapasha mubashara mamilioni ya waafrika majumbani kwao juu ya kitachokuwa kinajiri nchini Ivory Coast,”