Mastaa nane wanaosaka 'machimbo'
Muktasari:
- Sasa Guerreiro amehusishwa na AC Milan, ambayo inaweza kumsajili kama mbadala wa Pervis Estupinan anayehusishwa na Aston Villa. Iwapo atahamia Milan, kuna uwezekano mkubwa wa kurejea kucheza zaidi nafasi yake ya asili ya beki wa kushoto.
LONDON, ENGLAND: Zikiwa zimebaki takribani wiki nne kabla ya kuanza kwa msimu mpya wa ligi za ndani wa 2026-27, kuna majina makubwa ya wachezaji ambao bado hawajapata klabu mpya.
Kwa wachezaji wengi wa soka, maandalizi ya msimu tayari yameanza, huku klabu zikikusanya vikosi na kuanza maandalizi ya miezi 10 mingine ya ushindani katika mashindano mbalimbali.
Hata hivyo, siyo wachezaji wote ambao wana klabu mpya. Baadhi yao mikataba yao ilimalizika mwishoni mwa msimu uliopita na sasa wanaendelea kutafuta timu zitakazowapa nafasi ya kuendelea na maisha yao ya soka.
Hawa ni wachezaji wanane wenye majina makubwa ambao kwa sasa wapo sokoni wakiwa huru.
Mohamed Salah
Salah alikuwa na msimu wa 2025-26 ambao haukufikia viwango vyake vya juu vya kawaida, lakini bado alifanikiwa kufunga mabao 12 na kutoa pasi 10 za mabao katika mashindano yote.
Msimu mmoja kabla, 2024-25, alikuwa katika kiwango bora zaidi, akihusika moja kwa moja katika mabao 57 baada ya kufunga 34 na kutoa asisti 23. Pia, kwenye Kombe la Dunia 2026, Salah aliendelea kuonyesha kuwa bado ana uwezo wa kucheza katika kiwango cha juu.
Aliisaidia Misri kufika hatua ya 16 bora, ambako walikaribia kuiondoa Argentina iliyofika fainali. Katika mashindano hayo, ni wachezaji sita pekee waliotengeneza nafasi nyingi zaidi kutokana na mchezo wa wazi kuliko Salah, aliyefikisha nafasi 12, huku wote wakiwa wamecheza mechi nyingi zaidi yake.
Salah bila shaka ni mchezaji anayevutia klabu nyingi. Kwa muda alihusishwa na Besiktas ya Uturuki, lakini mpango huo unaonekana kuvunjika. Kwa sasa, klabu za MLS na Saudi Pro League ndizo zinazotajwa zaidi kama vituo vinavyoweza kuwa vya nyota huyo.
Dusan Vlahovic
Kwa ujumla, Vlahovic alifunga mabao 68 katika mechi 168 akiwa Juventus. Alifunga zaidi ya mabao 10 katika kila msimu wake minne kamili akiwa Turin, ingawa hakuwahi kufikisha mabao 20. Msimu wake bora ulikuwa 2023-24 alipofunga mabao 18.
Majeraha yamekuwa yakimzuia mshambuliaji huyo wa Serbia kufikia kiwango chake halisi. Msimu uliopita, jeraha la misuli ya paja lilimfanya acheze mechi 26 pekee katika mashindano yote, lakini bado alifanikiwa kufunga mabao 12.
Kuondoka kwake Juventus kunaonekana kuchangiwa zaidi na masuala ya mshahara kuliko uwezo wake wa kisoka. Kwa timu inayohitaji mshambuliaji mwenye uwezo wa kufunga mabao na yenye uwezo wa kumudu gharama zake, Vlahovic anaweza kuwa chaguo zuri.
Hata hivyo, historia yake ya majeraha inaweza kuzifanya baadhi ya klabu kuwa na mashaka. Amehusishwa na Besiktas, huku Barcelona pia ikiripotiwa kumuangalia kama mbadala wa Robert Lewandowski.
Jadon Sancho
Miaka michache iliyopita, wengi wangetabiri kuwa Kombe la Dunia 2026 lingekuwa jukwaa la Jadon Sancho, mwenye umri wa miaka 26, kung’ara. Lakini ukweli ni kwamba hakuwahi hata kuwa kwenye mjadala wa kuingia katika kikosi cha England cha kocha Thomas Tuchel.
Baada ya kuhamia Ujerumani mapema katika maisha yake ya soka, Sancho aling’ara akiwa Borussia Dortmund. Katika misimu yake mitatu, alihusika katika mabao 102 katika mechi 125, akifunga 49 na kutoa asisti 53.
Kiwango hicho kilimfanya Manchester United kumsajili mwaka 2021 kwa Pauni 73 milioni, lakini maisha yake Old Trafford hayakwenda kama ilivyotarajiwa. Katika mechi 83 za United, alifunga mabao 12 na kutoa asisti sita.
Vipindi vya mkopo akiwa Dortmund, Chelsea na Aston Villa pia havikurejesha Sancho kwenye kiwango chake bora. Sasa anatafuta klabu mpya baada ya mkataba wake kumalizika. Akiwa na miaka 26 pekee, bado kuna timu zinazoamini zinaweza kumrudisha kwenye ubora wake. Borussia Dortmund ndiyo klabu inayohusishwa zaidi na uwezekano wa kurejea kwake Ujerumani.
Leon Goretzka
Miaka minane iliyopita, Goretzka alijiunga na Bayern Munich kutoka Schalke 04 kama mchezaji huru. Tangu wakati huo, amekuwa sehemu ya kikosi kilichoshinda mataji makubwa, ikiwemo mataji saba ya Bundesliga, Kombe la DFB-Pokal mara tatu, Super Cup ya Ujerumani mara nne, Ligi ya Mabingwa Ulaya, UEFA Super Cup na Kombe la Dunia la Klabu.
Akiwa Bayern, Goretzka alipitia vipindi vya kupanda na kushuka chini ya makocha mbalimbali kama Hansi Flick, Julian Nagelsmann, Thomas Tuchel na Vincent Kompany. Hata hivyo, kila alipoonekana kupoteza nafasi au kiwango, mara nyingi aliweza kurejea kwa nguvu.
Akiwa na umri wa miaka 31, bado anaonekana kuwa na uwezo wa kusaidia timu kubwa. Msimu uliopita Bundesliga alifunga mabao matano na kutoa asisti tatu. Uzoefu wake mkubwa unamfanya kuwa mchezaji anayevutia klabu zinazotafuta kiungo mwenye uwezo wa kucheza katika kiwango cha juu. Amehusishwa na AC Milan, Juventus na Arsenal.
Franck Kessie
Kessie alijijengea jina kubwa Serie A akiwa Atalanta na AC Milan kabla ya kuhamia Barcelona na baadaye Al-Ahli. Sasa kuna uwezekano kiungo huyo wa Ivory Coast akarejea Italia.
Inaweza kuonekana kama Kessie amekuwa kwenye soka la juu kwa muda mrefu, lakini bado ana umri wa miaka 29 pekee. Alionyesha kwenye Kombe la Dunia 2026 kuwa bado ana uwezo wa kucheza katika kiwango bora.
Kessie ni mchezaji mwenye nguvu, uwezo wa kushinda mipira na uzoefu mkubwa. Pia ana uwezo mkubwa wa kupiga penalti. Akiwa Milan msimu wa 2020-21, alifunga penalti 11 za Serie A, rekodi iliyomweka miongoni mwa wachezaji waliofunga penalti nyingi zaidi katika msimu mmoja kwenye ligi tano bora za Ulaya katika kipindi cha karibuni.
Juventus ndiyo klabu iliyohusishwa zaidi naye, lakini pia kuna taarifa kwamba anaweza kuungana tena na kocha wake wa zamani wa Atalanta, Gian Piero Gasperini, ambaye sasa yupo Roma.
Julian Brandt
Inashangaza kumuona Julian Brandt kwenye orodha hii pamoja na Mohamed Salah, hasa kwa sababu Liverpool iliwahi kumtaka mwaka 2017. Hata hivyo, baada ya ushauri kutoka kwa timu ya utafutaji vipaji ya klabu hiyo, Liverpool iliamua kuwa Salah angekuwa chaguo bora zaidi.
Sasa, akiwa na miaka 30, Brandt ameondoka Borussia Dortmund baada ya misimu saba na anatafuta changamoto mpya. Ingawa uwezekano wa Liverpool kumsajili kama mbadala wa Salah unaonekana kuwa mdogo, kuna tetesi kwamba anaweza kuhamia Ligi Kuu England, huku Leeds United ikiwa miongoni mwa klabu zinazomfuatilia.
Kwa jumla akiwa Dortmund, Brandt alicheza mechi 307, akifunga mabao 57 na kutoa pasi 67 za mabao. Uzoefu wake wa kucheza katika nafasi mbalimbali za kiungo na ushambuliaji unaweza kumfanya kuwa chaguo zuri kwa klabu inayotafuta mchezaji mwenye uwezo wa kutengeneza nafasi na kufunga.
Lorenzo Pellegrini
Mchezaji mwingine aliyeaga klabu yake baada ya miaka mingi ya huduma ni Lorenzo Pellegrini. Alianza maisha yake ya soka akiwa Roma kabla ya kuhamia Sassuolo kwa misimu miwili kati ya 2015 na 2017.
Alirejea Roma mwaka 2017 kupitia kipengele cha kumnunua tena mchezaji na baadaye akawa mmoja wa wachezaji muhimu wa klabu hiyo. Kwa jumla, akiwa Roma alifunga mabao 62 na kutoa asisti 58.
Baada ya miaka tisa tangu kurejea kwake Roma, sasa Pellegrini ameondoka na kuanza kutafuta changamoto mpya. Akiwa na uzoefu mkubwa wa Serie A na soka la kimataifa, bado anaweza kuwa chaguo la kuvutia kwa klabu inayohitaji kiungo mwenye uwezo wa kushambulia na kutengeneza nafasi. Juventus pia inahusishwa na uwezekano wa kumsajili.
Raphael Guerreiro
Raphael Guerreiro ni mchezaji ambaye amekuwa na mchango mkubwa karibu kila alikocheza. Baada ya kujijengea jina Ligue 1, alihamia Borussia Dortmund mwaka 2016, ambako alicheza mechi 224, akifunga mabao 40 na kutoa asisti 42.
Mwaka 2023 alifuata njia iliyokuwa imezoeleka kutoka Dortmund kwenda Bayern Munich kama mchezaji huru. Uamuzi huo ulikuwa wa kushangaza kwa sababu alikuwa na umri wa miaka 29, lakini Guerreiro alithibitisha kuwa alikuwa nyongeza nzuri kwa kikosi cha Bayern.
Nguvu yake kubwa ni uwezo wa kucheza nafasi mbalimbali. Mchezaji huyo wa kimataifa wa Ureno anaweza kucheza beki ya kushoto, beki ya kulia, kiungo wa kati na hata nafasi za winga. Kwa jumla akiwa Bayern alicheza mechi 95, akifunga mabao 14 na kutoa asisti saba.
Sasa Guerreiro amehusishwa na AC Milan, ambayo inaweza kumsajili kama mbadala wa Pervis Estupinan anayehusishwa na Aston Villa. Iwapo atahamia Milan, kuna uwezekano mkubwa wa kurejea kucheza zaidi nafasi yake ya asili ya beki wa kushoto.