Majeraha ya William Saliba Arsenal pigo
Muktasari:
- Saliba alipata tatizo hilo wakati wa mchezo wa nusu fainali ambao Ufaransa ilifungwa mabao 2-0 na Hispania, ambapo alishindwa kuendelea na mchezo na kutolewa kipindi cha pili.
LONDON, ENGLAND: ARSENAL imepokea taarifa mbaya baada ya beki wake tegemeo, William Saliba atalazimika kukaa nje ya uwanja kwa hadi miezi mitano kutokana na majeraha ya mgongo aliyoyapata akiwa na timu ya taifa ya Ufaransa kwenye Kombe la Dunia.
Saliba alipata tatizo hilo wakati wa mchezo wa nusu fainali ambao Ufaransa ilifungwa mabao 2-0 na Hispania, ambapo alishindwa kuendelea na mchezo na kutolewa kipindi cha pili.
Kwa mujibu wa taarifa kutoka gazeti la L'Equipe, beki huyo mwenye umri wa miaka 25 anatarajiwa kufanyiwa upasuaji na huenda akarejea uwanjani mwezi Desemba.
ALISIKIKA AKILALAMIKA MAUMIVU
Tukio hilo lilitokea wakati Saliba alipokuwa akikimbia na mpira katika eneo lake bila kushinikizwa na mpinzani.
Ghafla alisimama, akaanguka chini na kuutoa mpira nje ya uwanja kabla ya kuonekana akimwambia beki mwenzake, Dayot Upamecano:"Mgongo wangu umeisha... mgongo wangu umeisha."
Baada ya hapo alishindwa kuendelea na nafasi yake ikachukuliwa na Maxence Lacroix.
PIGO KUBWA KWA ARTETA
Iwapo taarifa hizo zitathibitishwa, itakuwa habari mbaya kwa kocha Mikel Arteta ambaye alikuwa akijiandaa kuanza msimu mpya wa 2026/27 akiwa na matumaini ya kutetea ubingwa wa Ligi Kuu England.
Kutokuwepo kwa Saliba kutamaanisha Arsenal itakosa mmoja wa mabeki wake muhimu kwa miezi ya mwanzo ya msimu.
Arsenal inatarajiwa kuanza rasmi kampeni mpya kwa kuivaa Manchester City katika mchezo wa Ngao ya Jamii kabla ya kufungua msimu wa Ligi Kuu England dhidi ya Coventry City Agosti 21.
ALIKUWA AKICHEZA AKIWA NA MAUMIVU
Wakati wa hatua ya makundi ya Kombe la Dunia, Saliba mwenyewe alikiri kuwa alikuwa akiendelea kucheza licha ya kusumbuliwa na maumivu ya mgongo kwa miezi kadhaa.
"Nimekuwa nikipambana na maumivu madogo kwa miezi kadhaa. Nilivumilia kwa sababu kulikuwa na Ligi ya Mabingwa, Ligi Kuu na baadaye Kombe la Dunia."
Ameongeza:"Kombe la Dunia hufanyika mara moja tu kila baada ya miaka minne, hivyo nililazimika kuvumilia. Sikuwa kwenye asilimia 100 ya utimamu, lakini sikuwa nataka kutoa visingizio."
MSIMU ULIOPITA ALING'ARA
Msimu wa 2025/26, Saliba alicheza mechi 50 katika mashindano yote akiwa mmoja wa nguzo muhimu za Arsenal.
Aliisaidia klabu hiyo kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu, huku pia ikifika fainali za Ligi ya Mabingwa Ulaya na Kombe la Carabao.
Akiwa na Ufaransa kwenye Kombe la Dunia, alianza mechi mbili za hatua ya makundi, akapumzishwa mchezo wa tatu baada ya timu kufuzu hatua ya mtoano, kabla ya kurejea na kucheza mechi zote za hatua za mtoano hadi alipoumia dhidi ya Hispania.
Sasa macho ya mashabiki wa Arsenal yatakuwa kwa madaktari wa klabu hiyo, wakisubiri kujua kama beki huyo ataweza kurejea mapema au atakosekana hadi mwishoni mwa mwaka.