Msama: Tamasha la Pasaka mambo yote yapo sawa, nyie tu
Ikiwa imebaki siku moja kufanyika kwa tamasha la Pasaka uongozi wa kampuni inayoandaa tamasha hilo umesema kila kitu kinaenda vizuri.
Hayo yamesemwa leo Jumamosi Aprili 8, 2023 na Mkurugenzi wa Kampuni ya Msama Promotion, Alex Msama ambao ndio waandaji wa tamasha hilo alipozungumza na waandishi wa habari.
Msama amesema tayari wataalam wa kufunga majukwaa wapo katika viwanja vya Leaders ambapo tamasha hilo litafanyika na muda si mrefu wasanii watapanda jukwaani kujaribisha mitambo na sauti.
"Niwaambie tu wanachi maandalizi ya tamasha hilo kila kitu kinaenda sawa maandalizi kama mnavyoyaona, yaani mambo ni moto wao tu miguu yao kuja hapa" amesema Msama
Tamasha hilo la bure kwa mwaka huu linafanyika ikiwa imepita miaka saba halijafanyika pamoja na mambo mengine litatumika katika kumpongeza na kumuombea Rais Samia Suluhu Hassan kwa kufikisha miaka miwili madarakani.
Mgeni rasmi katika siku hiyo anatarajiwa kuwa Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari Nape Nnauye.
Waimbaji mbalimbali wanatarajiwa kuburudisha wakiwemo kutoka ndani na nje ya nchi kati yao yupo
John Lisu, Upendo Nkone Zablon Singers, Jesca BM, Beatrice Mwaipaja, Ambwene Mwaisonge na Tumaini Akilimali kwa Tanzania.
Kwa nchi za jirani yupo Fastinie Munishi na Tumaini Akilimali wa Kenya, Masi Masilia wa nchini Congo na Joshua Ngoma wa nchini Rwanda