Derby haikunoga kiviiile!

Muktasari:

TOFAUTI na siku nyingine inapokuwapo kwa mechi ya Kariakoo Derby, jana mambo yalipoa na hata wafanyabiashara waliojiimu mapema Uwanja wa Benjamin Mkapa, walijikuta wakishindwa kupiga hela kama ilivyozoeleka kutokana na uwanja pambano hilo kudorora.

TOFAUTI na siku nyingine inapokuwapo kwa mechi ya Kariakoo Derby, jana mambo yalipoa na hata wafanyabiashara waliojiimu mapema Uwanja wa Benjamin Mkapa, walijikuta wakishindwa kupiga hela kama ilivyozoeleka kutokana na uwanja pambano hilo kudorora.

Hata mashabiki waliojitokeza mapema jana walikuwa wachache kulinganisha na mechi zilizopita za Derby na hata zile za matamasha ya klabu hizo kongwe nchini, kwani hadi saa 7 mchana hali ilikuwa tete.

Baadhi ya mashabiki walisema derby ya jana ilipoozoeshwa na kiingilio kikubwa kwa majukwaa ya mzunguko ambayo wamekuwa wakitozwa kati ya Sh 5,000-7,000 tofauti na jana kutakiwa kulipia Sh10,000, huku vingine vikiwa ni Sh20,000 na 30,000 kilichokuwa cha juu zaidi.

Wakizungumza nje ya viwanja vya Benjamin na Uhuru, wafanyabishara walikuwa wakilalamika kutofanya biashara kwa tija kama inapokuwapo pambano kubwa kama hilo la watani.

Steven Joseph anayeuza jezi alisema viingilio vilivyowekwa na Shirikisho la Soka (TFF) kwa ajili ya mchezo wa jana ndio iomechangia kwa sehemu kubwa kufanya idadi ya mashabiki kuwa ndogo na wao kushindwa kupiga fedha kama siku nyingine za mechi kama hizo.

“Kwa kweli biashara leo (jana) imekuwa ngumu kwani mashabiki waliokuja uwanjani kutazama mchezo huu ni wachache, tatizo ni bei za viingilio wengi wamezoea kuingia kwa Sh5000, lakini leo ni Sh10,000, pia hata uhamasishaji haukuwa kama derby iliyopita ama matamasha ya klabu hizo, ” alisema Joseph.

Naye Anna Juma anayeuza chakula nje ya Uwanja wa Mkapa alisema biashara kwake ilikuwa ngumu sana kwani muda ulikuwa unaenda, huku akiwa na wateja wachache, wakati mechi kubwa kama hizo huwa anamaliza mapema msosi hata kama huongeza kipimo kikubwa cha chakula anachokiuza.

“Leo (jana) hali sio nzuri vyakula ni vingi sana mara nyingi katika mechi zinazowakutanisha Simba na Yanga muda kama huu (saa 7 mchana) chakula ndio tunamalizia, ila kwa sasa chakula bado kingi lakini tunajipa imani kwani mechi inapigwa saa 11 jioni,” alisema Anna akiungwa mkono na wenzake.

Achna na mashabiki wachache walioshindwa kuwanga mkono wafanyabiashara, lakini hata ndani ya uwanja mpaka saa 9 alasiri kulikuwa na mapengo makubwa ya mashabiki kutokana na idadi ndogo iliyojitokeza kulinganisha na Kariakoo Derby nyingine zilizopita kwa muda huo au ilivyokuwa kwenye Simba Day na Kilele cha Wiki ya Mwananchi na nyomi na amshaamsha zilianza mapema asubuhi kabla ya Kwa Mkapa kujazwa mapema hata kabla ya saa 8 mchana.

Mwanaspoti lililowahi mapema uwanjani hao lilishuhudia upande wa Kaskazini ambao wanakaa mashabiki wa Simba kulikuwa na eneo kubwa lisilo na mashabiki kama ilivyokuwa upande wa Kusini wanakokaa wenzao wa Yanga.

Licha ya kuwepo kwa burudani uwanjani hjapo kutoka kwa wasanii mbalimbali akiwamo Young Dee, TMK Wanaume Family na wengine, lakini uwanja ulishindwa kujazwa mapema na kundi kubwa lilionekana nje ya uwanja, baadhi wakilalamikia ukubwa wa viingilio.

“TFF ni kama wamefanyia tamaa mchezo huu, kwani hawakupaswa kuweka viingilio vikubwa kwa mechi ya Ngao ya Jamii, pia safari hii kumekuwa na uhamasishaji mdogo, pengine ni kwa vile mechi hiyo haisimamiwi na klabu japo Simba ndio iliyokuwa wenyeji wa mchezo, siku nyingine wajifunze,” alisikika akisema shabiki mmoja alioyekataa kutaja jina lake.

Hakuna kiongozi yeyote wa TFF, aliyepatikana kabla ya mchezo huo kuanza ili kutoa ufafanuzi juu ya malalamiko hayo ya mashabiki kwamba ukubwa wa viingilio hasa kwa majukwaa mzunguko yamechangia wengi wao kupata fursa ya kuujaza uwanja mapema, huku wale waliotoka mikoani wakionekana kufurahia kuja kushuhudia pambano hilo.


MZEE NA BAISKELI

Shabiki wa Yanga, Idd S.S. Mkuu jana alikuwa gumzo kabla ya pambano la watani baada ya kutinga uwanjani hapo na baiskeli aliyodai amesafiri umbali za zaidi ya kilomita 600 kwa muda wa siku nne kutoka jijini Arusha. Umbali huo aliosafiri shabiki huyo kwa basi huwa si chini ya saa 10.

Mkuu alisema ujio wake kwa baiskeli ulikuwa na ishara tosha ya ushindi kwa timu hiyo dhidi ya watani wao waliokuwa wakivaana nao kwenye pambano la Ngao ya Jamii kuzindua msimu mpya wa Ligi Kuu Bara inayoanza rasmi kesho.

Shabiki huyo alisema katika safari hiyo ya siku nne mfululizo alikutana na changamoto kadhaa ambazo alikabiliana nazo ilimradi kufanikisha kuja kulionda pambano hilo lililokuwa la saba kwa timu hizo katika michuano hiyo ya Ngao ya Jamii.

“Wakati nipo njiani nilikutana na mashabiki wa Simba walinizomea sana kutokana na mavazi ya Yanga niliyovaa, lakini haikunikatisha tamaa bali niliendelea na Safari yangu mpaka leo kufika hapa,” alisema Mkuu ambaye pia alisafiri na baiskeli hadi mkoani Kigoma kushuhudia fainali ya Kombe la ASFC na chama lake la Yanga kupasuka kwa bao 1-0 lililofungwa na kiungo Mganda, Taddeo Lwanga.