Job ataka rekodi Yanga

Job ataka rekodi Yanga

BAADA ya Yanga kutwaa ubingwa wake wa kwanza Ligi Kuu Bara, beki wa timu hiyo, Dickson Job amepanga kuweka rekodi mbalimbali akiwa ndani ya jezi ya Wanajangwani hao.

Job alijiunga na Yanga kwenye dirisha dogo la msimu uliopita akitokea Mtibwa Sugar kwa mkataba wa miaka miwil na kuingia moja kwa moja kikosi cha kwanza akicheza kama beki wa kati sambamba na nahodha Bakari Mwamnyeto.

Tangu aingie Yanga, mchezaji huyo ametwaa mataji matatu akianza na Kombe la Mapindizi msimu uliopita, Ngao ya Jamii mwanzoni mwa msimu huu na sasa Ligi Kuu, lakini nahodha huyo wa zamani wa timu za taifa za vijana Serengeti Boys na Ngorongoro Heroes ameeleza anataka rekodi zaidi akiwa Yanga.

“Nafurahi kuwa hapa, nataka niweke rekodi nyingi nikiwa na timu hii, tayari tumetwaa ubingwa bila kupoteza mechi hata moja, tupo fainali ya Kombe la Shirikisho pia tunataka kumaliza ligi bila kupoteza mechi,” alisema Job na kuongeza;

“Moja ya vitu vizuri kwa mchezaji ni kushinda mataji. Nahitaji kufanya hivyo kila niwezavyo ili kuwa na rekodi bora zaidi na kwa uwezo wa mungu naamini nitatimiza hilo.”

Kwa msimu huu, Job amekuwa mhilimili wa Yanga kwenye eneo la ulinzi ambapo mara nyingi amekuwa akicheza beki ya kati na Mwamnyeto au Yanick Bangala na baada ya kutwaa Ngao ya Jamii, ligi na sasa imebakiza fainali ya Kombe la Shirikisho (ASFC) itakayochezwa Julai 2 dhidi ya Coastal Union.