Pogba akiondoka, Ndombele anatua

MANCHESTER, ENGLAND

NI hivi, Manchester United imeweka wazi kwamba itakwenda moja kwa moja kwa kiungo Tanguy Ndombele kama supastaa wake, Paul Pogba ataamua kuchukua virago vyake na kuihama Old Trafford.

Man United imeonekana bayana kuhitaji huduma ya kiungo huyo wa Lyon, ambaye amekuwa na msimu bora kabisa huko kwenye klabu hiyo ya Ligue 1.

Lakini uhamisho wa Ndombele utacheleweshwa kidogo ukimsubiri Pogba afanye uamuzi wake, lakini ukichelewa sana itakula kwao.

Pogba, aliyenaswa kwa Pauni 89 milioni amekuwa haeleweki kwenye kikosi hicho akidai kwamba ndoto zake ni kwenda Real Madrid jambo linalomfanya Kocha Ole Gunnar Solskjaer kushindwa kufanya mipango yake kwa wakati.

Pogba alisema anataka kwenda Real Madrid hasa kwa kipindi hiki ambacho Zinedine Zidane amerudi kwenye kikosi hicho huko Bernabeu.

Lakini staa huyo wa kimataifa wa Ufaransa ameambiwa kama anataka kutua Bernabeu basi ni lazima aandike maombi ya kutaka kuondoka huku Man United ikiweka wazi mpango wake wa kwenda kumsajili Ndombele.

Man United inataka kusajili kiungo kuziba pengo la Ander Herrera, lakini kuhusu Ndombele itakuwa kwenye vita kali dhidi ya Paris Saint-Germain na vigogo wengine kama Real Madrid ambao wanavutiwa na huduma ya staa huyo wa Ligue 1.