Yanga yaikwepa Simba kijanja

Muktasari:

Simba na Yanga hizo zimekuwa zikitumia wiki hizo kufanya matukio mbalimbali kwa jamii, kutambulisha wachezaji wapya, jezi na bidhaa mpya za klabu.

WAKATI mabingwa wa Ligi Kuu Bara Simba wakitangaza kuanza kwa wiki ya Simba ambayo awamu hii itatambulika kama (Champions week another level), ambayo itaanza kufanyika kesho Ijumaa Agosti 14, Yanga wameamua kufanya mabadiliko ya tarehe.

Wiki hiyo ya Simba, itafikia kilele Agosti 22, kwa kucheza mechi na kutambulisha wachezaji wao wapya waliowasajili msimu huu pamoja na wale ambao walikuwa nao katika kikosi hiko kama utamaduni wao ulivyo.

Yanga wametangaza kufanya SportPesa Wiki ya Mwananchi 2020 ambayo itazinduliwa Jumamosi Agosti 22, Dodoma badala ya Agosti 15 kama ilivyokuwa imepangwa hapo awali.

Taarifa iliyotolewa na klabu hiyo kupitia mtandao wa kijamii wa Twitter imesema sababu kubwa ya kusogeza mbele ni kutoa muda wa kutosha kwa wanachama, mashabiki na wapenzi wa Yanga kutoka katika maeneo mbalimbali ya nchi yetu kuhudhuria ufunguzi huo.

“Aidha kamati ya hamasa, kamati tendaji na wadau wote wa kamati ya maandalizi ya wiki ya Mwananchi inawakaribisha wote kuhudhuria uzinduzi huu wa kihistoria katika Mji mkuu wa nchi, Dodoma” umesomeka ujumbe huo