VIDEO: Goli la Morrison lilivyomtesa aliyekuwa Waziri wa Fedha

Muktasari:

Saada Mkuya alikuwa Waziri wa Fedha wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuanzia Januari 2014 hadi Novemba 2015


Dodoma. Waziri wa zamani wa Fedha wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Saada Mkuya amefichua kuwa aliteswa vilivyo na kipigo cha bao 1-0 ambacho Simba ilikipata kutoka kwa Watani wao Yanga, Machi 8 mwaka huu.

Akizungumza jijini Dodoma leo, Mkuya alisema baada ya kipigo hicho alikosa raha kwa siku kadhaa ingawa baadaye alikubaliana na matokeo hayo.

"Sijatoka nyumbani kwa sababu mimi kuna rafiki yangu wa karibu yeye ni Yanga kwa hiyo sikutoka nyumbani halafu akawa ananitumia zile 'emoji' yaani nikawa simjibu. Simjibu mpaka tulivyokuwa tumepoa," alisema Mkuya ambaye kwa sasa ni Mbunge wa Jimbo la Welezo.

Bao hilo pekee la ushindi la Yanga katika mchezo huo lilifungwa na mshambuliaji Bernard Morrison kwa mkwaju wa faulo.

Mkuya amefichua kuwa yeye ni shabiki damu wa Simba na pia Manchester United.

"Mimi ni Simba damu halafu ni mpenzi wa Manchester United. Maana yake 'in such a way' kwamba siku Manchester United inacheza, mimi sitaki niangalie. Yaani ni kusikia matokeo kama tumefungwa, tumeshinda basi.

Kama tunashinda basi nitaangalia 'previews' tu. Siwezi kuhimili kuona aidha inafungwa. Naweza kama nikiwa na 'confidence' tutashinda lakini hiyo 'confidence' kwa kipindi cha karibuni imeondoka," alisema Mkuya.