Wabunge kuifuata Taifa Stars Misri

Muktasari:

  • Katika Fainali za Mataifa ya Afrika mwaka huu ambazo zinafanyika Misri, Stars itafungua dimba dhidi ya Senegal na baadaye itacheza na Kenya huku mechi ya mwisho ikiwa dhidi ya Algeria

Dar es Salaam.Wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wamepanga kuelekea Misri kwa ajili ya kuiunga mkono timu ya taifa 'Taifa Stars' inayoshiriki Fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON) zinazofanyika nchini humo kuanzia Juni 21 hadi Julai 19.

Akizungumza Bungeni leo, Spika wa Bunge, Job Ndugai alisema kuwa leo ndio siku ya mwisho kwa wabunge wanaotaka kwenda Misri kujiorodhesha na umeandaliwa utaratibu maalum wa kuwawezesha kufanikisha hilo.

"Tumeona sio vyema kwa vijana kuwa peke yao kule hivyo tumepanga kwenda kuungana nao. Nimepata taarifa kuwa wenzetu wa Burundi na Uganda wanajipanga kwenda kwa wingi kule Misri na pia tuna mechi dhidi ya Kenya hivyo haitopendeza kuona wenzetu wanaspoti vijana wao na sisi hatupo.

Wabunge ambao wako tayari kwenda Misri, leo baada ya kikao wanatakiwa wabaki hapahapa ili tupeane utaratibu. Na tukiwa kule Misri nadhani tutapata fursa ya kwenda kutembelea vivutio vya utalii pamoja na kutembelea Bunge la Misri.

“Kikubwa wale walio tayari kusafiri wanatakiwa waandae hati zao za kusafiria pamoja na picha tatu ili waandaaji waanze kushughulikia hiyo safari," alisema Spika Ndugai.

Spika alisema kati ya nafasi 34 za kusafiri kwenda Misri kupitia Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere jijini Dar es Salaam, nafasi tano tayari zimeshajazwa na sasa zimebakia nafasi tisa tu.