Vidal na Inter kumalizana leo

INTER Milan ipo kwenye nafasi kubwa ya kuipata saini ya kiungo wa Barcelona, Arturo Vidal na ripoti zinadai kuwa mwamba huyo atakuwa Italia kufanya vipimo vya Afya leo kabla ya kusaini kandarasi ya kuitumkia miamba hiyo ya Jiji la Milan.

Inaelezwa kuwa Inter inataka kumsainisha mkataba wa miaka miwili ambao utamfanya kukunja Euro 6 milioni kwa mwaka na kocha Antonio Conte amemfanya kuwa chaguo lake la kwanza kwenye orodha ya viungo ambao alitarajia kuwasainisha katika dirisha hili.

Vidal anaondoka Barcelona baada ya kocha, Ronald Koeman kumwambia kuwa hana mpango wa kumtumia katika kikosi chake kwa msimu ujao, hivyo amemfungulia mlango wa kutokea.

Fundi huyo kutoka Chile mkataba wake unatarajiwa kumalizika mwaka 2021 na thamani yake katika soko la usajili ni Euro 11 milioni.

Safari ya mwamba huyo kutoka Taifa la Chile kwenda Italia limeanza tangu jana na sasa kinachobaki kwa staa huyo kumalizana na mabosi Inter Milan inayoendelea kupambana kuimarisha kikosi chake kwaajili ya mapambano ligi.