Valverde atupiwa virago, Barcelona yatangaza kocha mpya

Muktasari:

  • Klabu ya Barcelona imemtangaza Quique Setien kuwa kocha mpya wa timu hiyo kujaza nafasi ya Ernesto Valverde aliyefukuzwa.

Madrid, Hispania. Barcelona imemtangaza kocha mpya Quique Setien kujaza nafasi Ernesto Valverde aliyefukuzwa.

Valverde aliondoka Athletic Bilbao kwenda kuinoa Barcelona mwaka 2017 kabla ya jana kutupiwa virago licha ya timu hiyo kuongoza katika msimamo wa Ligi Kuu Hispania.

Muda mfupi baada ya Barcelona kumtimua, Valverde, klabu hiyo imemg’oa Setien kutoka Real Betis.

Valverde (55), anaondoka Nou Camp akiwa ameipa Barcelona ubingwa wa Ligi Kuu Hispania mara mbili.

Miongoni mwa sababu zilizochangia kocha huyo kufukuzwa ni kushindwa kucheza mchezo wa fainali ya Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Msimu uliopita Valverde alikuwa katika presha kubwa baada ya Barcelona kupata matokeo yasiyoridhisha katika mechi za Ligi Kuu na Ligi ya Mabingwa Ulaya.

Setien (61), ametia saini mkataba wa miaka miwili na nusu na leo atatambulishwa kwa waandishi wa habari.

“Tumekubaliana na Valverde kuvunja mkataba kwa manufaa ya pande zote mbili, tunamshukuru kwa kazi nzuri katika kipindi chote alipokuwa katika familia ya Barca,”ilisema taarifa ya klabu hiyo.

Awali, nahodha wa zamani wa Barcelona Xavi Hernandez alikuwa akipewa nafasi ya kuteuliwa kocha baada ya kuzungumza na Mkurugenzi wa Ufundi wa Eric Abidal na Mtendaji Mkuu Oscar Grau kabla ya kukaa ombi hilo.