TFF waibuka na hili uchaguzi Yanga ufanyike

Muktasari:

Wakati TFF ikikomalia uchaguzi Yanga, baadhi ya wanachama wa kikosi hicho akiwemo Katibu Mkuu wa Tawi la Yanga Ubungo Terminal, Stephen Mwakilema amesema kitendo cha Shirikisho hilo kusimamia uchaguzi wao bila ya kuwa na rejea ni kuvunja katiba ya klabu yao.

 

Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Ally Mchungahera amesema zoezi la usaili linatarajia kuisha leo Ijumaa huku wagombea wote wa juu wakiwa tayari wamefanyiwa usaili.

Akizungumza na Mwanaspoti, Mchungahera alisema wameongeza siku moja baada ya baadhi ya wagombea kuomba kutokana na kuwa nje ya nchi na wanatarajia kurudi siku hiyo kabla haijamalizika.

Amesema wagombea wote watatu wanaogombea nafasi ya Mwenyekiti na wanne wa nafasi ya Makamu Mwenyekiti wameshasailiwa.

"Wajumbe ni asilimia chache iliyobaki ambao bado hawajasailiwa japo siwezi kukwambia muda huu ni kinanani kwani muda wa kumaliza bado haujaisha kwa siku ya leo," alisema.

"Kumekuwa na taarifa kwamba tunawapitisha wagombea kugombea nafasi hizo bila kufahamu kama ni wanachama hai si za kweli wanachama wanakuja na barua kutoka katika matawi yao na kadi zao za uanachama wakiwa wameshazilipia kwa kuonyesha na risiti,"alisema Mchungahela.

Ameongeza kuwa wanatarajia kutumia reja kuwatambua wanachama wanaogombea nafasi mbalimbali za uongozi klabuni hapo na watakao piga kura Januari 13.