Simba wajiunga kupinga ubaguzi wa rangi

Muktasari:

Klabu ya Simba imekuwa timu ya kwanza nchini kutumia alama kama ishara ya kupinga ubaguzi wa rangi kutokana na kifo cha  Floyd ambacho  kimesababisha maandamano makubwa Marekani na kuzua taharuki duniani kote.


ASUBUHI  ya leo Simba wameungana na klabu mbalimbali kubwa barani Ulaya ikiwemo Chelsea  na Liverpool kupinga tukio la ubaguzi wa rangi na mauaji ambayo alifanyiwa Mmarekani  mweusi George Floyd, Mei 25 huko Minnesota na Polisi wa nchi hiyo.

Kabla ya kuanza kwa  mazoezi ya leo asubuhi, wachezaji wa Simba, wametengeneza alama ya kupiga goti moja ikiwa ni ishara ya kutoa ujumbe wa kutaka haki itendeke kwa watu wote pasipo ubaguzi wowote wa  rangi.

Wachezaji hao wa Simba, walipangwa na wasimamizi wao ili kupata umbo ambalo  lilibeba ujumbe wa kupinga ubaguzi wa rangi wa 'imetosha sote ni binadamu'.

Tofauti na Chelsea ambao walitengeneza alama H wakiwa na maana ya 'Humans' kwa Simba haikuwa hivyo kwani kila mchezaji alitakiwa awe sehemu ya ujumbe bila kuzingatia kuchora kama ilivyokuwa kwa klabu nyingine.

Wachezaji wa  Liverpool  wenyewe walizunguka mduara wa kati kati ya uwanja na  kupiga goti, ikiwa na maana sote ni binadamu tunapaswa kuwa wamoja.

Floyd ambaye ni raia mweusi wa Marekani ambaye kifo chake kimesababisha maandamano makubwa Marekani, alikufa kutokana na ukosefu wa hewa safi  kwa mujibu wa uchunguzi wa maiti yake.

Alifariki kwa kukandamizwa kwa goti shingoni na mgongoni na maafisa wa polisi wa Minnesota, uchunguzi wa kimatibabu uliosimamiwa na familia ya Floyd umebaini hilo.