Sarpong, Carlinhos wamaliza utata

Muktasari:

Katika mchezo huo Yanga walihaha kupata bao, lakini mshambuliaji Michael Sarpong aliwainua mashabiki wote waliokuwa Uwanja wa Azam Complex.

ZILIKUWA dakika 37 tu alizotumia winga Carlos Fernandes 'Carlinho' kuwanyanyua mashabiki wa Yanga baada ya kutumia pasi yake ndefu iliyoenda kuzaa bao la ushindi katika mchezo wao wa kirafiki dhidi ya Mwadui uliomalizika 1-0 katika Uwanja wa Azam Complex, jana usiku.

Carlinho aliingia kipindi cha pili dakika 45 akichukua nafasi ya Juma Mahadhi na mabadiliko hayo yalizaa matunda baada ya kupata bao la ushindi.

Katika mchezo huo dakika 83 Carlinho alitumia pasi ndefu ya juu juu ambayo ilienda kukutana na mshambuliaji, Michael Sarpong ambaye alionyesha sio mchezaji wa kukata tamaa baada ya kupambana na beki wa Mwadui, Joram Mgeveke aliyejichanganya na kipa wao kisha Sarpong kuuwahi mpira na kuupiga ulioenda moja kwa moja wavuni.

Goli hilo liliibua shangwe uwanja mzima kutokana na namna ambavyo mshambuliaji Michael Sarpong alionyesha maana halisi ya upambanaji kwani kama angekuwa mtu wa kukata tamaa asingefunga goli hilo.

Carlinho amekuwa na kawaida ya kuzalisha mabao ya namna hiyo licha kwamba uwanjani anakuwa hana kashikashi sana ya kupambana na mabeki wa timu pinzani.

Kwa upande wa Mwadui goli hilo lilitaka kuwamaliza nguvu kwani walipambana katika dakika zote na kuonyesha kuhitaji goli, lakini kulikuwa na changamoto kutoka kwa mabeki wa Mwadui.

Yanga ni kama vile walikata kiu ya mashabiki wao waliokuwa uwanjani kwani walikuwa wanasikika wakihitaji bao la ushindi katika mchezo huo.

Kikosi cha Yanga kimezidi kucheza mchezo wa kufunguka na kupiga pasi za haraka haraka tangu katika mchezo wao wa mwisho wa Ligi Kuu dhidi ya Coastal Union waliposhinda 3-0.