Ni fainali ya JKT, Magereza ndondi taifa

WAKATI klabu ya JKT Makao Makuu (MMJKT) ikiingiza mabondia 13 kwenye fainali ya mashindano ya ngumi ya Taifa, Magereza imeingiza mabondia watatu huku kocha wake, Anthony Kameda akisisitiza kuwa fainali hiyo itakuwa ya kufa mtu.

Mabondia 20 watapanda ulingoni leo Ijumaa Agosti 07,2020 kuanzia saa tisa alasiri kusaka ubingwa wa mashindano hayo yanayofikia tamati kwenye viwanja vya Tanganyika Packers, Kawe Dar es Salaam katika uzito tofauti.

Katika uzani wa bantam, John Mchonga wa Magereza atazichapa na Hussein Juma wa MMJKT na Godfrey Samwel wa Magereza atacheza na Alex Sita wa MMJKT kwenye uzani wa super heavy.

"Hii itakuwa ni zaidi ya fainali, tutapambana kufa na kupona kutwaa ubingwa," amejinasibu bondia wa zamani wa timu ya taifa na kocha, Anthony Kameda wa Magereza.

Mazimbu Ally wa MMJKT alidai kati ya mabondia wake 13 waliotinga fainali, ana uhakika medali zote za dhahabu watachukua kutokana na maandalizi waliyofanya.

Mapambno mengine, Abdallah Mohamed wa MMJKT atazichapa na Hamad Hashim wa Iringa.

Uzani wa fly, fainali itawakutanisha mabondia wote wa MMJKT, Issa Omari na Innocent sawa na kwenye uzani wa light ambapo atazichapa Mwarami Mganda na Hassan Mrutu na kwenye uzani wa light welter ambapo atazichapa Sebastian John na Shaba Mganda.

Wengine, Mohamed Juma atacheza na Gurushadi Rashid na Haruna Sinundo atacheza na SUled Rashid katika uzani wa middle.

Kwenye uzito wa light heavy, Justine Chota wa Magereza atazichapa na Musa Changarawe wa Mwanza na John Mchonga wa Magereza atacheza na Hussein Juma wa MMJKT.