Yanga, Simba, Azam kuwasha moto wa Ligi Kuu Tanzania Bara Krismasi

Muktasari:

Awali ratiba ya Ligi Kuu ilikuwa inaonyesha Simba, Yanga na Azam hazitokuwa na mchezo wowote mpaka mwakani, lakini kwa mujibu wa ratiba mpya iliyotolewa Bodi ya Ligi inaonyesha watacheza mechi mbili kila moja kabla ya kufunga mwaka.

Dar es Salaam.Vigogo wa soka Simba na Yanga watacheza mechi zao la Ligi Kuu Tanzania Bara katika siku kuu Krismasi kwa mujibu wa ratiba mpya ya ligi hiyo kabla ya mchezo wao wa watani wa jadi utakaopigwa Januari 4, 2020.

Awali ratiba ya Ligi Kuu ilikuwa inaonyesha Simba, Yanga na Azam hazitokuwa na mchezo wowote mpaka mwakani, lakini kwa mujibu wa ratiba mpya iliyotolewa Bodi ya Ligi inaonyesha watacheza mechi mbili kila moja kabla ya kufunga mwaka.

Mwanaspoti baada ya kupata ratiba hiyo yenye marekebisho, ilimtafuta Afisa Mtendaji mkuu wa Bodi ya Ligi, Boniface Wambura na alisema wamebadili kutokana na ratiba za mashindano mengine kubadilika.

"Tarehe za mashindano ya Kombe la Chalenji Cecafa zimebadilika," alisema kwa kifupi.

Kwa mujibu wa ratiba inayonyesha Desemba 24, Yanga watakuwa jijini Mbeya kucheza dhidi ya Mbeya City wakati mabingwa wa Ligi Kuu Bara wenyewe watashuka uwanja siku ya Krismasi Desemba 25 kuivaa Lipuli kwenye Uwanja wa Uhuru.

Yanga watashuka tena kwenye Uwanja wa Sokoine, Desemba 27 kuivaa Tanzania Prisons wakati Desemba 28, KMC watakuwa wenyeji wa Simba kwenye Uwanja wa Uhuru.

Baada ya hapo Simba na Yanga zitapata wiki moja ya kujianda kwa kabla ya mchezo wao wa watani wa jadi utakaopigwa Januari 4, kwenye Uwanja wa Taifa.

Mabingwa wa Kombe la FA, Azam watakuwa wageni wa Polisi Tanzania Desemba 24, na siku tatu baadaye watasafiri hadi Tanga kuivaa Coastal Union kwenye Uwanja wa Mkwakwani Desemba 27.