Eymael akomaa na Mwamvuli, Cioaba aloana Azam yaitangulia Yanga 1-0

Muktasari:

Makocha hao wawili wasimama muda wote kuwaelekeza wachezaji wao namna ya kukaba na kushambulia katika mchezo huo uliopoteza mvuto kutokana na mvua hizo.

Dar es Salaam. Mvua zinazoendelea kunyesha zimempa wakati mgumu kocha wa Yanga, Luc Eymael akilazimika kutumia mwamvuli huku mwenzake wa Azam FC, Aristica Cioaba amekubalia kuloana na mvua wakati wakitoa maelekezo kwa wachezaji.

Makocha hao wawili wasimama muda wote kuwaelekeza wachezaji wao namna ya kukaba na kushambulia katika mchezo huo uliopoteza mvuto kutokana na mvua hizo.

Kocha wa Yanga, Eymael alikuwa akipata tabu kutoa maelekezo akiwa na mwamvuli wakati Cioaba yeye hakujali mvua hiyo kumnyeshea.

Katika dakika ya 25, Azam FC imepata bao 1-0 la kuongoza baada ya beki wa Yanga, Ally Sonso kujifunga wakati akijaribu kuokoa mpira wa kona uliokolewa na kipa wake Farouk Shikalo.

Jambo hilo lilimkera kocha wa Yanga ambaye alizunguka nyuma ya benchi huku akiwa anatikisa kichwa kutokana na timu yake kuwa nyuma ya bao 1-0.

Baada ya kurejea sehemu yake ya kusimama ili kuendelea kuwaelekeza wachezaji upepo ukampitia na kufanya mwamvuli wake kujikunja akabaki anahangaika nao.

Akasaidiwa na watu ambao walikuwa wamekaa benchi kuuweka sawa mwamvuli wake kisha kuendelea kuutumia.

Kocha huyo alikuwa akitaka kuwaelekeza wachezaji alikuwa anamuita Charles Mkwasa kuongea na wachezaji.

Molinga awakosha mashabiki

Pamoja na Yanga kuwa nyuma kwa bao 1-0, mshambuliaji David Molinga alikuwa akijituma akisaka mpira kutokea katikati ya dimba mpaka ndani ya 18.

Molinga anatumia nguvu kulazimisha mashambulizi na wakati mwingine anapiga mashuti ya mbali, lakini yanashindwa kuzaa matunda.