Mwananchi ilivyozindua promosheni ya ‘TAJIRIKA na eGazeti’
Muktasari:
- Promosheni ya TAJIRIKA na eGazeti inakuja wakati ambapo huduma ya kusoma magazeti mtandaoni iliyopewa jina la eGazeti ikiwa na miezi mitatu lakini kwa muda mchache tu ina watumiajia zaidi ya 70,000 ndani na nje ya nchi.
Dar es Salaam. Kampuni ya Mwananchi Communications Limited (MCL) ambao ni wachapishaji wa magazeti ya Mwananchi, The Citizen, Mwanaspoti na pia watoa huduma kupitia njia mbalimbali za mtandaoni imezindua rasmi promosheni maalumu inayofahamika kama TAJIRIKA na eGazeti.
Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam leo Jumanne, Juni 30, 2020 Mkurugenzi Mtendanji wa MCL, Francis Nanai amesema promosheni hiyo inalenga kuwazawadia wasomaji wake, ambao kwa muda mrefu wamekuwa nao tangu kuanzishwa kwa magazeti yanayochapishwa na kampuni ya MCL hadi sasa ambapo unaweza kusoma magazeti mtandaoni kwa urahisi na kwa bei nafuu.
Promosheni hii inakuja wakati ambapo huduma ya kusoma magazeti mtandaoni iliyopewa jina la eGazeti ikiwa na miezi mitatu lakini kwa muda mchache tu ina watumiajia zaidi ya 70,000 ndani na nje ya nchi.
eGazeti ni mfumo bora wa kusoma magazeti mtandaoni ya MCL. Ili uweze kusoma magazeti hayo unachotakiwa kufanya ni kupakua App ya eGazeti kwenye Google Playstore au tembelea www.egezeti.co.tz.
Kwa kutumia mfumo wa eGazeti unayasoma magazeti kutoka MCL kwa urahisi na kwa bei nafuu ikiwemo kifurushi cha Shilingi 1,000 tu ambacho unasoma nakala ya Mwananchi, The Citizen na Mwanaspoti.
Nanai amesema Tanzania ni nchi kubwa na kwa kutumia Tehama na wabunifu wa hapa hapa ndani ya nchi wameweza kufanikisha eGazeti na kuwawezesha Watanzania kusoma nakala zao popote walipo ambapo mitandao inapatikana.
Kwa upande wake Mhariri Mtendaji Mkuu wa MCL, Bakari Machumu alisisitiza kuwa, lengo la MCL ni kuhakikisha kuwa wasomaji wa magazeti ya Mwananchi, The Citizen na Mwanaspoti wanapata habari zilizo bora na zinazokwenda na wakati na pia zilizofanyiwa utafiti na uchambuzi wa kina.
Pia Mkuu wa Idara ya Biashara wa MCL, Kenneth Mugabe amesema katika promosheni hiyo kutakuwa na zawadi mbalimbali ikiwa ni pamoja na zawadi za kila siku, wiki na za mwisho wa promosheni.\
Zaidi ya Sh100milioni zitashindaniwa. Sh20 milioni kila mwezi, Sh5 milioni kila wiki na Sh1 milioni kila siku na kubwa kuliko ni Sh20 milioni atakayoondoka nayo mshindi wa jumla katika droo kubwa ya mwisho wa promosheni baada ya miezi mitatu.
Droo za kila wiki zitakuwa zinarushwa kupitia chaneli ya YouTube ya Mwananchi Digital kila Jumanne saa nne kamili asubuhi kuanzia Juni 7, 2020.