Mwakinyo asepa na kijiji

Muktasari:

Mwakinyo atazichapa na Tinampay wa Ufilipino katika pambano la raundi 10 la uzani wa super welter litakalopigwa kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

WAKATI pambano la Hassan Mwakinyo dhidi ya Arnel Tinampay likitarajiwa kupigwa Novemba 29, bondia huyo unaambiwa amesepa na kijiji huko Tanga.

Huko Tanga kwenye kambi ya Mwakinyo kazi ndiyo kwanza imeanza, kwani jamaa wamepanga kumsindikiza Mfaume Mfalme kwa msafara wa Coster kama tano kwa ajili ya pambano la hilo.

Bondia huyo atazichapa na Keisy Ally katika pambano la utangulizi sanjari na Twaha Kiduku ambaye atacheza dhidi ya bondia kutoka Urusi.

Mwakinyo atazichapa na Tinampay wa Ufilipino katika pambano la raundi 10 la uzani wa super welter litakalopigwa kwenye Uwanja wa Uhuru, Dar es Salaam.

“Ni kweli maandalizi ya mashabiki kwenda Dar es Salaam yameanza kwa kujiandikisha na kulipia usafiri,” alisema Mwakinyo.

Alisema atawasili Dar es Salaam na mashabiki hao ambao wamejitolea kumsindikiza kwenye pambano hilo.

Wakati hali ikiwa hivyo, pambano la Mfaume na Ally ni kama mechi ya Simba na Yanga kutokana na uhasimu wa makocha wao ambao wanatoka kambi za Mabibo na Manzese. Kambi hizo zimeendelea kujifua kujiandaa na kipute hicho.