Mwakinyo: Bondia yeyote nitakayeletewa halali yangu

Muktasari:

Mwakinyo anatarajiwa kuzichapa kuwania ubingwa wa IBU Afrika kwenye uzani wa super welter.

Dar es Salaam. Wakati wasimamizi wa Hassan Mwakinyo wakifanya mazungumzo na mabondia wawili wa nje ya nchi ili wazichape na bondia huyo Agosti 8, Mwanamasumbwi huyo amesema yuko tayari kumkabili yoyote atakayeletewa.

Mwakinyo anatarajiwa kuzichapa kuwania ubingwa wa IBU Afrika kwenye uzani wa super welter.

Akizungumza na Mwanaspoti, Mwakinyo alisema maandalizi ya awali ya pambano hilo linalotarajiwa kupigwa kwenye ukumbi wa Mlimani City yameanza.

Amesema tayari amepewa taarifa ya kucheza na aidha bondia wa Afrika Kusini au raia wa DR Congo anayeishi Afrika Kusini.

"Sijaambiwa majina yao,lakini 'management' yangu imeeleza mmoja kati ya mabondia wanaoishi nchini humo ndiyo nitacheza naye," anasema.

Anasema licha ya kufichwa jina la mpinzani wake, lakini yuko tayari kumkabili yeyote atakayeletwa mbele yake.

"Najiamini na mazoezi kwangu ni kama ibada, sijawahi kuacha.Niko kambini chini ya kocha wangu Hamis (Mwakinyo ambaye ni kaka yake) tayari kwa maandalizi ya ubingwa," amesema.

Bondia huyo ambaye aliwahi kuwa namba 16 duniani kwenye uzani wa welter kabla ya kuporomoka amesema pambano hilo litakuwa njia ya yeye kurejea upya kwenye ubora wake.