Mo Salah afichua kitu kuhusu Klopp

Muktasari:

Mo Salah amesema Klopp amewaambia wachezaji wake wote kuhakikisha wanafanya vizuri kwenye kila michuano kushinda msimu ujao ili kubeba kila taji.

CAIRO, MISRI. SUPASTAA wa Misri, Mohamed Salah amefichua kile ambacho kocha wao huko Liverpool, Jurgen Klopp amekuwa akiwaambia kuhakikisha msimu huu wanaweka kibindoni kwanza taji la Ligi Kuu England.

Mo Salah alishuhudia ubingwa huo wa msimu uliopita ukienda kwa Manchester City kwa tofauti ya pointi moja tu na hivyo kuendelea kusubiri kwa miaka kibao taji hilo, wakishindwa kulibeba tangu lilipoanzishwa miaka 30 iliyopita.

Liverpool walimaliza msimu na pointi 97, lakini walimaliza uchungu baada ya kwenda kubeba ubingwa wa Ligi ya Mabingwa Ulaya, walipoichapa Tottenham Hotspurs kwenye mchezo wa fainali uliofanyika Madrid, Hispania.

Mo Salah amesema Klopp amewaambia wachezaji wake wote kuhakikisha wanafanya vizuri kwenye kila michuano kushinda msimu ujao ili kubeba kila taji.

“Kuendelea kupambana kama tunataka kushinda kitu msimu huu, tufanye kuliko msimu uliopita. Kupambania mataji yote msimu huu,” alisema.

Mo Salah anafichua kwamba, Klopp amewapiga marufuku kugusa maandishi ya ‘This is Anfield’ yaliyoandikwa kwenye mlango wa kuingilia kwenye korido ya uwanjanni Anfield, akiwaambia wasifanye hivyo, hadi hapo watakaposhinda ubingwa.

“Unapocheza klabu kama Liverpool, siku zote matarajio yanakuwa makubwa, lakini ushindi kitu,” alisema Mo Salah.