Kinda Hudson-Odoi atoa masharti kwa Chelsea

Muktasari:

 Mchezaji huyo amesema hatamwaga wino hadi ahakikishiwe namba katika kikosi cha kwanza vinginevyo ataondoka. 

London, England. Callum Hudson-Odoi ametoa masharti kwa klabu yake ya Chelsea kabla ya kutia saini mkataba mpya.

Mchezaji huyo amesema hatamwaga wino hadi ahakikishiwe namba katika kikosi cha kwanza vinginevyo ataondoka.

 Hudson-Odoi anawindwa na klabu za Ulaya baada ya kucheza kwa kiwango bora msimu uliopita.

Mazungumzo ya Chelsea na winga huyo kinda mwenye miaka 18 kuhusu mkataba mpya yanaendelea.

Mchezaji huyo amesita kuongeza mkataba kwa kuhofia kusugua benchi msimu ujao.

Hudson-Odoi alionyesha mchezo mzuri baada ya kocha Maurizio Sarri  kumpa nafasi katika kikosi cha kwanza ambapo alifunga mabao matano kabla ya kuumia katika mechi dhidi ya Burnley.

“Callum  hana tamaa ya fedha, jambo muhimu kwake ni kupata  namba kikosi cha kwanza, vinginevyo hatakubali kutia saini,”kilisema chanzo cha karibu na mchezaji huyo.

Kigogo cha soka Ujerumani Bayern Munich imeonyesha dhamira ya kutaka saini yake majira ya kiangazi.