Kasi ya Kagere yamtia presha Aiyee

Muktasari:

Salim Aiyee ameitazama kasi ya staa wa Simba, Meddie Kagere kisha akasema msimu huu anaona kama atafanya maajabu zaidi ya yale alioonyesha msimu ulioisha

Dar es Salaam. Meddie Kagere ameanza kumpasua kichwa straika wa KMC, Salim Aiyee baada ya kutupia mabao mawili Simba ikishinda 3-1 dhidi ya JKT Tanzania, mechi ya ufunguzi.

Msimu ulioisha Aiyee alimaliza nafasi ya tatu katika orodha ya wafungaji bora wa Ligi Kuu akiwa amefunga mabao 18, huku Kagere akiwa kinara kwa magoli 23.

Aiyee yupo nje kutokana na kusumbuliwa na nyonga, kitendo cha Kagere kuanza na mabao mawili katika ufunguzi wa ligi kuu Bara kimempa hofu na kuona atakuwa na mlima mrefu wa kukimbizana naye.

Aiyee alisema Kagere ni mshambuliaji anayempa changamoto tangu msimu ulioisha, jambo ambalo anaamini msimu huu utakuwa na ushindani zaidi wa kuzifumania nyavu.

"Kwa haraka haraka msimu huu naona mshambuliaji anayeweza kuwa tishio tena ni Kagere, nilitazama mechi ya Simba na JKT Tanzania, nimeona kasi ya jamaa kama inaongezeaka"

"Kagere anajua anataka nini kwenye soka, ndio maana huwezi kumhukumu kwa umri wake kama anafanya maajabu tofauti na vijana ambao walitakiwa kufanya kitu hawajafanya"

"Natamani nipone haraka ili nirejee katika malengo yangu, kwani sikutegemea ningekumbana na mkasa wa kusumbuliwa na nyonga, nitapambana natamani kuvunja rekodi yangu mwenyewe,"alisema Aiyee.