Jahazi la Wazito laenda mrama, Hall aomba muda

Muktasari:

Toka msimu ulipoanza, klabu hiyo imeshuhudia mabadiliko kibao kwenye safu  ya uchezaji. Tayari bwanyenye wa Kiitaliano anayoimiliki ameshawafuta kazi makocha wanne lakini bado hali haikubadilika.

Nairobi, Kenya.KOCHA wa klabu tajiri nchini Wazito FC, Stewart Hall kaomba apewe muda katika kipindi hiki anachojaribu kuunda kikosi kipya kabisa.

Kwenye dirisha la usajili la Januari lililokamilika hivi majuzi, Wazito walisajili zaidi ya wachezaji nane wapya lakini bado wameendelea kuzalisha matokeo ya kuvunja moyo.

Hata hivyo kulingana na kocha Hall, jambo hilo ni la kawaida ikizingatiwa kwamba ni kipndi cha mpito na wengi wa wachezaji wake ni wapya hivyo  bado hawajaweza kujeli kama inanvyotakiwa.

“Kwa sasa  tupo katika kipindi cha mpito. Tunaunda kikois kipya kabisa ukizingatia nkwamba tuliwaachia wachezaji 10 na kusajili tisa. Hapa tunazungumzia timu mpya kabisa hivyo itatuchukua muda kuiva na kuwa dhabiti lakini ninachoweza kusema ni kuwa tayari tumeshika mkondo huo”

Kwenye mechi ya wikendi, walitoka sare ya kufungana goli 1-1 dhidi ya Kakamega Homeboyz, wakiwa wamefuatisha matokeo hayo na kipigo cha magoli 3-0 walichopokezwa na Posta  Rangers.

Toka msimu ulipoanza, klabu hiyo imeshuhudia mabadiliko kibao kwenye safu  ya uchezaji. Tayari bwanyenye wa Kiitaliano anayoimiliki ameshawafuta kazi makocha wanne lakini bado hali haikubadilika.

Hapo ndipo akaamua kumpa kazi Hall ambaye amekuwa akifanya safisha safisha ya kikosi kwa  kuwatema wachezaji walioondoka ili kutwaa nafasi kwa wengine wapya. Kwa sasa wanagandia katika nafasi ya 14, wakiwa wameshinda mechi mbili pekee.