Dk Tulia abeba jimbo la Sugu

Muktasari:

Dk Tulia ameshinda kwa jumla ya kura 75, 225 dhidi ya wagombea wengine watano wa vyama vya upinzani.

 

Mgombea ubunge kwa tiketi ya CCM, Dk Tulia Ackson, ametangazwa mshindi wa ubunge katika jimbo la Mbeya Mjini.

Dk Tulia ameshinda kwa jumla ya kura 75,225 na kuibuka kidedea dhidi ya wagombea wengine watano wa vyama vya upinzani akiwamo mgombea wa Chadema, Joseph Mbilinyi 'Sugu' aliyepata kura 37,591.

Matokeo yametangazwa asubuhi hii ya Alhamisi Oktoba 29, 2020 na Msimamizi Mkuu wa Jimbo la Mbeya Mjini, Amede Ng'wanidako katika ukumbi wa Mkapa jijini Mbeya.

Wagombea wengine ni Protas Mgaimbila wa Chaumma aliyepata kura 236, Mwakaje Kaili (NCCR-Mageuzi) kura 206 na Rafael Ngonde (CUF) aliyepata kura 88.

Sugu alikuwa akitetea kiti hicho kwa muhula wa tatu, baada ya kuliongoza jimbo hilo tangu mwaka 2010 alipompokea Benson Mpesya wa CCM.