Bocco achimba mkwara mzito

Muktasari:

  • Akizungumzia mchezo huo, Bocco alisema ni fursa kwa Simba na wachezaji wake kuitangazia dunia kwamba, Tanzania kuna vipaji vya soka vuya uhakika.

MABINGWA watetezi wa Ligi Kuu Bara, Simba ndio wanajipanga kuvaana na wababe wa La Liga, Sevilla hapo Mei 23, mwaka huu, kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Lakini, kama hufahamu ni kuwa mchezo huo unasubiriwa kwa hamu kubwa na nahodha wa Simba, John Bocco, ambaye amesema watautumia kunadi vipaji vya Tanzania kimataifa.

Pia, amesema kamwe hawatakuwa wanyonge na badala yake watapambana kuhakikisha wanashinda ili kudhihirisha wako vizuri kwelikweli msimu huu.

Sevilla itatua nchini Mei 21 ikiwa na kikosi chake kamili na Mei 23 itashuka Uwanja wa Taifa kuikabili Simba. Ziara ya wababe hao wa La Liga inaratibiwa na kampuni ya michezo ya kubahatisha, SportPesa Tanzania kwa kushirikiana na La Liga pamoja na Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).

Akizungumzia mchezo huo, Bocco alisema ni fursa kwa Simba na wachezaji wake kuitangazia dunia kwamba, Tanzania kuna vipaji vya soka vuya uhakika.

Pia, alisema kuwa wanajiona wenye bahati kubwa kupata nafasi hiyo ya kujipima na Sevilla na kwamba, wanaishukuru SportPesa kwa kuratibu ziara hiyo nchini.

“SportPesa ndio wadhamini wetu na kwa hili wanastahili pongezi kubwa kwani, kuileta Sevilla ambayo imewahi kutwaa ubingwa wa Europa ni fursa adimu sana,î alisema Bocco.

Hata hivyo, alisema kuwa kama TP Mazembe, Al Ahly, AS Vita walitulizwa kwenye Uwanja wa Taifa basi Sevilla watatulizwa mapema tu.

Naye kipa wa Sevilla, Tomas Vaclik alisema wamejipanga kufanya vyema katika mchezo huo licha ya kuwa ni wa kirafiki kwani, watashusha kikosi kamili.