Bocco, Fraga mbona freshi!

NAHODHA wa Simba, John Bocco mara baada ya kumaliza mechi na Mtibwa Sugar hakuonekana tena uwanjani kutokana majeruhi lakini sasa amerejea na mzuka wote.

Bocco alikosa michezo mitatu iliyopita lakini hata katika mechi ya Biashara United pia akaumia goti kiungo Mbrazil, Gerson Fraga.

Mwanaspoti lilimtafuta Daktari wa Simba, Yassin Gembe akasema Bocco anaendelea vizuri na ameshaanza mazoezi mepesi chini ya uangalizi wa kocha wa viungo, Adel Zrane na mtalaamu wa misuli, Paul Gomez.

Gembe alisema maendeleo ya kiafya ambayo ameonyesha Bocco huku akiwa anafanya programu ya mazoezi ambayo kila siku inabadilika, siku si nyingi atajiunga na wenzake pamoja na kocha mkuu, Sven Vandenbroeck kuendelea na ratiba zilivyo.

“Kuhusu Fraga anaendelea na matibabu taratibu ili kurudi kwenye utimamu kwanza wa mwili na baada ya hapo ataendelea na hatua inayofuata, ila kwa sasa bado kwanza yupo chini ya uangalizi,” alisema Gembe.

Katika hatua nyingine kocha wa viungo, Zrane alisema: “Bocco yupo vizuri tangu tumeanza programu ya kufanya mazoezi pembeni, ameonekana kuwa tayari bila shida jambo ambalo muda si mrefu nitampa ruhusa ya kujiunga na wenzake na kuona namna gani anaweza kwenda kutumika katika mechi.”

“Kuhusu Fraga bado hajafika kwangu, kwa maana hiyo nadhani yupo katika matibabu ambayo anaendelea nayo tangu hapo awali na akionekana kuwa na mwelekeo mzuri atafika katika programu yangu na kumuandaa ili aweze kurudi pamoja na wenzake,” alisema.