Arteta: Tunapiga hatua zaidi mbele

 London, England. Kocha wa Arsenal, Mikel Arteta anaamini kikosi chake kimepiga hatua kwa kuifunga Liverpool kwa mikwaju ya penalti na kutinga hatua ya robo fainali ya Kombe la Carabao.

Baada ya kwenda suluhu kwa dakika 90 kwenye Uwanja wa Anfield, kipa wa Gunners, Bernd Leno alipangua penalti mbili, kabla ya Joe Willock kufunga.

Arsenal ilichapwa mabao 3-1 kwenye mechi ya Ligi Kuu England na Liverpool siku nne zilizopita, naArteta ameridhishwa na mchezo wa juzi suiku.

“Tuna safari ndefu bado, lakini kwa sasa inaonekana tumepiga hatua,” alisema kocha huyo raia wa Hispania.

“Hii ni mara ya tatu katika wiki nane tumecheza na timu bora za Ulaya, kwa upande wangu, hii ni hatua kubwa mbele kwa timu yangu.

“Tunataka kucheza kila mashindano kama nafasi kwetu ya kutwaa taji, tunatakiwa kulifanya hilo, tutacheza na kufanya makubwa.”

Timu hizo zilipata matokeo ya 5-5 kabla ya Liverpool kushinda kwa penalti msimu uliopita.