Adi Yusuf anatisha kwa mijengo mjue

Muktasari:

  • Adi alisema apartments hizo zipo 12 zinapangishwa na kukodishwa kwa yeyote mwenye uhitaji wa kuzitumia na familia yake kutoka sehemu yoyote duniani.

INAWEZEKANA straika mpya wa Blackpool, Adi Yussuf aliwaza na kuwazua kuwa maisha yake yatakuwaje baada ya kustaafu soka, majibu yakamjia la msingi ni kuwekeza kwenye mijengo ‘apartments’ za kisasa.

Jamaa ni mjanja kinoma, baada ya kucheza soka kwa kipindi kirefu ameamua kufanya uwekezaji kwenye mijengo hiyo ambayo watalii au mtu binafsi unaweza kwenda kupumzika ukiwa na familia yako.

Katika kuhakikisha anawanasa watalii, mijengo ya Adi ipo Tanga na Arusha karibu na vivutio vya kitalii.

Adi alisema apartments hizo zipo 12 zinapangishwa na kukodishwa kwa yeyote mwenye uhitaji wa kuzitumia na familia yake kutoka sehemu yoyote duniani.

“Nilikaa na kuwaza nikaona inafaa kufanya kitu cha namna hii, ilinichukua muda kufanya uamuzi lakini naona nimefanya uamuzi sahihi,” alisema mshambuliaji huyo.

Nyota huyo kwa sasa yupo Misri na timu ya Taifa ya Tanzania ‘Taifa Stars’ kwenye maandalizi ya fainali za Mataifa ya Afrika (AFCON) 2019 zitakazoanza kutimua vumbi Juni 21 kwa mechi ya ufunguzi kati ya Misri na Zimbabwe.