Gadiel: Ubora wa Tshabalala ndio mafanikio yangu Simba

Muktasari:

Gadiel Michael anauchukulia ubora wa mshindani wake wa namba Mohemed Hussein 'Tshabalala' kumpa umakini wa kufanya kazi zake kwa viwango vya juu ili kufikia malengo yake ya kufika mbali.

Dar es Salaam. Beki wa Simba, Gadiel Michael amesema hana presha na ushindani wa namba dhidi ya Mohamed Hussein 'Tshabalala'akiamini kila mtu ana ubora wake ambao utapimwa uwanjani.

Gadiel amesema ubora wa Tshabalala ndio utakaomfanya asibweteke na kukalishwa benchi, hivyo anauchukulia kama kipimo cha kazi yake kujua ni yaina gani.

"Tshabalala ni beki mzuri ila pia ukimuuliza yeye kuhusu mimi atakwambia nipo vizuri, ushindani wetu ni mafanikio ya timu kufanya vyema na sio sisi tu hata safu zingine"

"Ndio maana unakuta wote wawili tunaitwa kwenye kikosi cha Taifa, hii kwetu ni nzuri kujituma ili kila mmoja kulinda kiwango chake, lakini kama mtu hana mshindani basi kuna vitu vinakuwa vinapungua"

"Kubwa zaidi nina malengo ya kufika mbali, hapa sio mwisho wangu, hivyo lazima nipite kwenye ushindani ambao utakuwa unanifanya niwe najituma kwa bidii"amesema.

Huu ni msimu wa kwanza kwa Gadiel kucheza Simba, ambayo ilimsajili kutoka Yanga, usajili wake ulitikisa kutokana na Wanajangwani bado walikuwa wanamhitaji wakapigwa bao na watani wao wa jadi.