Dully Sykes, Jaydee majaji wapya BSS, Idrissa Sultan mtangazaji

Muktasari:

Shindano hilo BSS mwaka huu litafanyika katika mikoa mitano, Arusha, Dar es Salaam, Dodoma, Mbeya na Mwanza limekuja na kauli mbiu ni 'kinyumbani zaidi ngoma inayeya'.

Dar es Salaam. Jaji Mkuu wa Shindano la Bongo Star Search (BSS) Ritha Poulsen ametangaza wanamuziki Dully Sykes, Lady Jaydee kuwa majaji wapya huku Idrisa Sultan akiwa mtangazaji wa shindano.

Shindano hilo BSS mwaka huu litafanyika katika mikoa mitano, Arusha, Dar es Salaam, Dodoma, Mbeya na Mwanza limekuja na kauli mbiu ni 'kinyumbani zaidi ngoma inayeya'.

Ritha alisema Dully Sykes na Lad Jaydee wataungana na jaji Mkongwe Master J pamoja na yeye.

Akizungumzia nafasi aliyopewa ya ujaji Dully Sykes alisema anashukuru kupata nafasi hiyo kwani anauwezo mkubwa na uzoefu katika muziki hivyo atatenda haki katika shindano hilo.

"Mimi sisemi sana, ila nashukuru kwa kuniaminiwa  sababu najua wameangalia vigezo na ukizingatia mimi nina miaka 20 katika muziki ninauwezo mkubwa wa kutambua kitu kizuri na kibaya na tutapiga kazi vizuri," alisema Dully Sykes.

Naye Lady Jaydee alisema amechaguliwa kutokana na uzoefu katika suala la muziki hivyo Watanzania wategemee kitu tofauti kutoka kwake.

"Ni jambo la kumshukuru Mungu kwa kupata nafasi hii kuwa jaji katika shindano la BSS, uzoefu ninao na uzuri muziki naufahamu vizuri, hivyo nawahaidi Watanzania nitaonyesha utofauti katika nafasi yangu ya ujaji," alisema Lady Jaydee.

Aidha Idrisa Sultan atakuwa mtangazaji wa shindano hilo alisema amekuwa na furaha kufanya kazi na watu sio tu wakongwe bali ni maarufu hivyo watu wajipange kuona ubunifu wake mpya katika utangazaji wa shindano hilo.

Master J alisema tangu shindano lianze amekuwa ni mmoja wa majaji, hilo ni jambo la kumshukuru Mungu na kushukuru uongozi wote wa shindano hilo.