Pigo KMC; Mugiraneza, Bokungu kuwakosa AS Kigali

Muktasari:

Matokeo ya ushindi wa aina yoyote ile yataivusha KMC hadi hatua inayofuata ya mashindano ya Kombe la Shirikisho Afrika

Dar es Salaam. Baadhi ya nyota wa kigeni wa klabu ya KMC wataikosa mechi ya marudiano ya Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya AS Kigali ya Rwanda mnamo Agosti 23.

Sababu ya nyota hao kukosa mechi hiyo ni kuchelewa kupatikana kwa leseni zao kutoka Shirikisho la Soka Afrika (Caf) pia kuchelewa kwa hati zao za uhamisho wa kimataifa (ITC).

Meneja wa KMC, Faraji Muya alisema kuwa uwezekano wa nyota hao kucheza mechi hiyo ni finyu kwa kuwa hawatoweza kupata nyaraka hizo kwa wakati.

"Hali ya kambi ni nzuri na molali ya wachezaji iko juu na maandalizi yanaendelea vyema.

Tutawakosa Mugiraneza ma Sivilwa (Melly) ambao bado wanasubiria leseni za Caf, lakini wachezaji wengine wako tayari kwa mchezo," alisema Meneja huyo.

Bokungu kwa upande wake ataukosa mchezo huo kutokana na kuchelewa kwa ITC yake wakati huohuo wakisubiria ripoti ya daktari kuona kama majeruhi wao Charles Ilanfya, Salim Aiyee na Abdallah Mfuko wanaweza kucheza au la.