Makocha wapewa akili Taifa Cup

Muktasari:
- Kibonajoro aliyasema hayo kutokana na kasumba iliyokuwepo ya viongozi wa mkoa, kutegemea wachezaji kutoka Mkoa wa Dar es Salaam.
Katibu mkuu wa chama cha mpira wa kikapu mkoa wa Kigoma Anasi Kibonajoro ameishauri mikoa iwe inatumia wachezaji wake katika mashindano ya Taifa Cup.
Kibonajoro aliyasema hayo kutokana na kasumba iliyokuwepo ya viongozi wa mkoa, kutegemea wachezaji kutoka Mkoa wa Dar es Salaam.
Alisema hata kama ni wazawa wa mkoa fulani, kuwatumia wachezaji wa mkoa husika kutaifanya mikoa iwe na maendeleo.
“Kwa kweli kutegemea wachezaji wa Dar es Salaam, kunaweza kupoteza nafasi ya kuonekana wachezaji wanaotoka katika mikoa,” alisema Kibonajoro.
Wakati huohuo, baadhi ya makocha kutoka mikoa ya Mara na Pwani na wengine wakiwatumia waakilishi wao, walionekana katika uwanja wa Donbosco Upanga wakifuatilia Ligi ya kikapu mkoa wa Dar es Salaam (BDL).
Makocha hao, walikuwa na lengo la kutafuta wachezaji watakaochezea mikoa yao katika mashindano ya Taifa Cup.
Mashindano ya Taifa Cup yamepangwa kuanza Juni 24, katika uwanja wa Chinangali, Dodoma.