AS Vita yatoa sababu za kutosa Wiki ya Mwananchi Yanga

Muktasari:

Yanga iliwalika AS Vita katika kucheza mchezo wa kirafiki katika tamasha lao la Wiki ya Mwananchi.

Dar es Salaam. AS Vita ya DR Congo imethibitisha sababu za kutokuja nchini kuumana na Yanga katika tamasha la Wiki ya Mwananchi iliyokuwa ifanyike Agosti 4, 2019 kwenye Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.

Kocha msaidizi wa AS Vita, Raul Shungu amesema ni kweli walikuwa waje Tanzania kucheza na Yanga, lakini sasa mpango huo umesitishwa.

Shungu ambaye amewahi kuifundisha Yanga amesema sababu ya kusitisha ziara hiyo ni kufuatia kutoka ratiba ya mechi za Ligi ya Mabingwa Afrika.

Shungu amesema ratiba ya CAF imeonyesha wanatakiwa kuanza kucheza mchezo wa kwanza ugenini wakiwafuata UMS de Loum ya Cameroon.

Kocha huyo amesema ratiba ya kutakiwa kucheza mechi hiyo Agosti 9 ndiyo imefuta zaidi kutokana kukaribiana zaidi na ratiba ya Yanga waliopanga wacheze nao Agosti 4.

Amesema tofauti ya siku tano baina ya mechi hizo mbili huku wakitakiwa kuanzia ugenini kwa kwenda a Cameroon ndiyo msingi wa kufutwa kwa ratiba hiyo.

Aidha Shungu amesema kufuatia ratiba yao hiyo pia imewalazimu kubadili ratiba ya maandalizi yao kwa kusitishwa kwa sehemu ya maandalizi yao.