Pazia la Miss Tanzania 2019 lazinduliwa Dar es Salaam

Muktasari:
Hii ni mara ya pili kwa kampuni ya The Look kuandaa shindano la Miss Tanzania baada ya waandaaji wa awali, Lino International Agency chini ya Hashim Lundenga kujiondoa.
Imani Makongoro
Dar es Salaam. Msimu mpya wa shindano la Miss Tanzanis 2019 umezinduliwa huku fainali zake zikitarajiwa kufanyika Agosti 23 jijini Dar es Salaam.
Mwenyekiti wa Kamati ya Miss Tanzania na Mkurugenzi wa The Look Company, Basilla Mwanukuzi amesema msimu huu mashindano hayo yatashirikisha pia mikoa ya Songwe, Simiyu, Kagera, Tanga na Shinyanga ambayo msimu uliopita haikushiriki.
Alisema mrembo wa mwaka huu ataiwakilisha nchi katika mashindano ya dunia yatakayofanyika Desemba 14, London, England.
"Baada ya mashindano ya mikoa na kanda, washiriki wataanza kambi ya Taifa kwa wiki tatu kabla ya fainali itakayofanyika kwenye ukumbi wa New Millennium Tower Makumbusho," alisema.
Basilla Miss Tanzania mwaka 1998 alisema Watanzania watakaopenda kwenda England kushuhudia fainali za dunia na kuongeza hamasa kwa mshiriki wa Taifa wawasiliane na na uongozi wa The Look.